TAARIFA KWA UMMA KUHUSU AJIRA MPYA ZA UALIMU
NA KADA ZA AFYA
1. UTANGULIZI
Ndugu Wanahabari;
Mtakumbuka kuwa mwezi Aprili, 2022; Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, alitoa
kibali cha ajira kwa kada za Ualimu na Afya, kwa ajili ya kuajiri
walimu 9,800 wa Shule za Msingi na Sekondari, na wataalam
wa Afya 7,612.
Baada ya kupata kibali cha ajira, Ofisi ya Rais – TAMISEMI ilitoa
tangazo kwa wahitimu mbalimbali wa Ualimu na Kada za Afya,
kuwasilisha maombi ya kazi, kupitia mfumo wa kielektroniki wa
kupokea na kuchakata maombi ya ajira, kuanzia tarehe
20/04/2022 hadi 08/05/2022. Jumla ya maombi 165,948
yakiwemo ya Wanawake 70,780 na Wanaume 95,168
yaliyopokelewa kwenye mfumo, ambapo maombi ya Kada za Afya
ni 42,558, na Kada ya Ualimu ni 123,390.
Ndugu Wanahabari;
Ili kufanikisha mchakato wa ajira, Ofisi ya Rais – TAMISEMI
iliunda Timu Maalum, ya kufanya Uchambuzi wa Maombi ya
Ajira, iliyohusisha Taasisi mbalimbali. Taasisi hizo ni pamoja na
Ofisi ya Rais Ikulu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa
Umma na Utawala Bora, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Ofisi ya
Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Wizara
ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania
(TCU), Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Ufundi Stadi (NACTVET), Sekretarieti ya
Ajira, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(TAKUKURU), na Mabaraza ya Kitaalamu katika Sekta ya Afya.
(a)Vigezo Vilivyotumika
Ndugu Wanahabari;
Kutokana na idadi ya waombaji kuwa kubwa, Timu ya
Uchambuzi wa Maombi ya Ajira ilipewa vigezo vilivyoandaliwa
kama mwongozo wa kutoa ajira kwa waombaji, kwa lengo la
kuhakikisha uwepo wa haki na uwazi katika zoezi hili. Katika
kuhakikisha usawa wa kijinsia unafikiwa, katika vigezo
vilivyotumika kupata waajiriwa wapya kwa mwaka 2022, kila
kigezo kilizingatia uwiano wa kijinsia. Vigezo vilivyotumika ni
kama ifuatavyo: -
i. Mwaka wa kuhitimu
Katika kigezo hiki, kipaumbele kimetolewa kwa waombaji wenye
sifa waliotangulia kuhitimu kwa mfuatano wa mwaka, kulingana
na hitaji la kada/kozi au kiwango cha Elimu, na pia mwaka wa
kozi ilivyoanza kutoa wahitimu.
ii. Umri wa kuzaliwa
Waombaji wenye sifa waliopangwa kwa mujibu kigezo namba (i)
hapo juu walipangwa kulingana na umri wa kuzaliwa. Lengo ni
kuwawezesha waombaji wenye umri unaokaribia miaka 45
kuingia katika utumishi wa umma kwa masharti ya kudumu,
kwa mujibu wa Sera ya Ajira Menejimenti na Ajira katika
Utumishi wa Umma toleo la Pili la mwaka 2008iii. Waombaji Wenye Ulemavu
Uchambuzi wa maombi ya watu wenye Ulemavu ulifuata vigezo
vyote vya mwaka wa kuhitimu na umri wa kuzaliwa,
vilivyooneshwa kwenye kipengele cha (i) na (ii). Hata hivyo, vigezo
hivi vilitumika kuwashindanisha waombaji wenye ulemavu peke
yao, kwa kuzingatia takwa la Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na.
9 ya mwaka 2010, kifungu cha 31 (1)-(3). Uchambuzi huu
ulifanywa kwa ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana,
Ajira na Watu wenye Ulemavu.
Ndugu Wanahabari
Mchakato wa uchambuzi wa maombi ya ajira ya Kada za Afya na
Ualimu ulizingatia utaratibu ufuatao:-
i. Kwanza, ilihusisha uchambuzi wa moja kwa moja kutoka
kwenye mfumo wa maombi. Mfumo huu umewezesha
waombaji wote wenye sifa kupata ajira kwa haki na usawa,
kama yalivyo maelekezo ya Rais wa Serikali ya Awamu ya
Sita, Mhe. Samia Suluhu Hassan, kwamba Watanzania
wote wenye Sifa wapate ajira bila upendeleo. Hivyo mfumo
huu uliwachuja waombaji awali kwa kuzingatia mahitaji ya
kibali cha ajira kilichotolewa, ukamilifu wa viambata
vilivyohitajika kwa mwombaji, na mwaka wa kuhitimu
waombaji; na
ii. Pili, uchambuzi wa kina ulifanyika ukihusisha pia uhakiki
wa nyaraka za maombi yaliyopata uzito wa juu, kulingana
na vigezo vilivyowekwa.
2. KUHUSU UZINGATIAJI WA MAHITAJI NA MSAWAZO
SAWA WA WATUMISHI
Ndugu Wanahabari
Upangaji wa watumishi wa Kada za Afya na Ualimu katika Vituo
vya kutolea huduma za Afya na shule, umezingatia mahitaji ya
watumishi katika mikoa husika. Kutokana na juhudi za
Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mhe. Samia Suluhu
Hassan, katika kufanya maboresho makubwa ya Sekta ya Afya,
upangaji wa watumishi wapya umezingatia mahitaji ya
watumishi katika Halmashauri zenye Hospitali mpya, Vituo vya
Afya vipya, na Zahanati mpya zilizokamilika ambazo
zimeshindwa kutoa huduma za msingi, kutokana na kukosa
watumishi wenye sifa, pamoja na Halmashauri zenye upungufu
mkubwa wa watumishi hao. Aidha, kwa upande wa kada za
Ualimu, utaratibu wa upangaji ulizingatia mgawanyo wa nafasi
kwa kila somo, na kiwango cha Elimu kulingana na hitaji la
kibali.
Mchakato huu wa ajira umetoa fursa kwa waombaji kutoka
mikoa yote ya Tanzania, hivyo basi upangaji wake umezingatia
uzalendo na utamaduni wetu, kuwa kila mtanzania anaweza
kufanya kazi mahali popote nchini.
3. WAOMBAJI WALIOKIDHI VIGEZO NA KUPANGIWA
VITUO
(a)Waombaji wa Kada za Afya
Ndugu Wanahabari
Kwa upande wa kada za Afya, Waombaji wenye sifa waliokidhi
vigezo na kupangiwa vituo vya kazi ni 6,876 wanawake ni 3,217
sawa na asilimia 46.8 na wanaume ni 3,659 sawa na asilimia
53.2 wakiwemo wenye ulemavu 42 sawa na asilimia 0.61
kutokana na uchache wa waombaji wenye sifa wa kundi hilo.
Aidha, nafasi 736 kada za Afya zilikosa waombaji wenye sifa.
Kada hizo ni Daktari wa Meno (50), Tabibu Meno (43), Tabibu
Msaidizi (244), Mteknolojia Mionzi (86) na Muuguzi- ngazi ya
cheti (313). Kada hizi zitarudiwa kutangazwa ili kupata waombaji
wenye sifa watakaojaza nafasi hizo.
Ndugu Wanahabari
Mchanganuo wa idadi ya wataalamu wa Kada za Afya waliopata
nafasi za ajira umeoneshwa kwenye Jedwali la 1.
(b)Waombaji wa Kada za Ualimu
4. SHUKRANI KWA MHE. RAIS
Ndugu wanahabari
Tunamshukuru sana Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kutekeleza
sera ya elimu bila ada, ambapo pamoja na mambo mengine,
imepelekea watoto ambao walikuwa hawawezi kusoma kutokana
na kushindwa kulipiwa ada, kwenda mashuleni. Kutokana na
ongezeko la wanafunzi kupitia sera hii, uhitaji wa walimu na
miundombinu ya madarasa umeongezeka. Katika kukabiliana
na changamoto hii, kwa kipindi cha miezi 15 aliyokuwepo
madarakani, Rais wetu mpendwa ametuwezesha kujenga
madarasa 15,000 kupitia fedha za mkopo wa IMF, na kutupatia
kibali cha kuajiri watumishi wa elimu 9,800 na wa afya 7612.
Aidha, katika mwaka 2020/21 Serikali iliajiri watumishi 23,000
kada ya elimu na afya. Hatua hizi zinazochukuliwa na Mhe.
Rais zinastahili kupongezwa sana.
5. MAELEKEZO YA WAZIRI
Ndugu wanahabari
Napenda kutumia fursa hii kutoa maelekezo ya Msingi
mbalimbali yanayopaswa kuzingatiwa na Waajiriwa na Waajiri.
a. Waajiriwa wapya wote wahakikishe wanaripoti
kwa Wakurugenzi wa Halmashauri walizopangiwa
wakiwa na Kitambulisho cha taifa au namba ya
utambulisho ya NIDA, Cheti halisi cha kuzaliwa,
Vyeti Halisi vyote vya Taaluma na Utaalamu wa
Kazi vya mwajiriwa, ili vihakikiwe na Mwajiri kabla
ya kupewa barua ya ajira;
b. Waajiri wote wahakikishe wanapokea vyeti na
kuviwasilisha baraza la mitihani kwa ajili ya
uhakiki. Wizara ipewe taarifa mara moja kwa wale
watakaokutwa na vyeti ambavyo ni vya kugushi
ili hatua kali zichukuliwe;
c. Waajiri wote wahakikishe watumishi wapya
waliopangwa kwenye Halmashauri, wanapewa
barua za ajira, na kuripoti kwenye vituo
walivyopangiwa tu, na si vinginevyo;
d. Mwajiriwa
mpya
atakayechukua
posho
ya
kujikimu, na baadaye asiripoti katika kituo chake
cha kazi alichopangiwa, atachukuliwa hatua
stahiki kwa mujibu wa sheria;
e. Waajiriwa wapya ambao hawataripoti katika vituo
walivyopangiwa ndani ya siku 14, kuanzia tarehe
ya tangazo hili, watakuwa wamepoteza nafasi zao
ambazo zitajazwa na waombaji wengine wenye sifa,
waliopo kwenye Kanzidata (Database) ya Ofisi ya
Rais – TAMISEMI;
f. Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa
ambazo
Waajiriwa
wapya
wamepangwa,
wahakikishe wanawapokea Waajiriwa wapya na
kuwawezesha kwa kuzingatia Sheria, Kanuni,
Taratibu na Miongozo ya Utumishi wa Umma, na
baadaye kutoa taarifa ya kuripoti kwao. Taarifa za
kuripoti waajiriwa hao zijazwe kwenye mfumo wa
kielektroniki (ajira.tamisemi.go.tz), baada ya kila
mtumishi kupokelewa na kukamilisha taratibu;
g. Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa
wanaelekezwa kukamilisha taratibu za ajira
haraka, ili waajiriwa wapya waingizwe kwenye
mfumo wa taarifa za kiutumishi na mishahara
(HCMIS) mapema iwezekanavyo;
h. Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wote
wa Halmashauri,
kuhakikisha
wanatekeleza
maagizo ya OR-TAMISEMI yaliyotolewa kwenu
Mwezi Machi, 2022, ya kuhakikisha mnafanya
msawazo wa IKAMA ya walimu wa Shule za Msingi
na Sekondari, ndani ya Mkoa na Halmasgauri
kabla au ifikapo tarehe 30 Juni, 2022. Tekelezeni
kwa biddi maelekezo hayo ili kuhakikisha shule
zinakuwa na uwiano mzuri wa walimu, na taarifa
ya utekelezaji iwasilishwe kabla au ifikapo tarehe
15 Julai, 2022. OR-TAMISEMI haitasita
kumchukulia hatua Mwajiri ambaye hatatekeleza
maelekezo haya ya kufanya msawazo wa walimu katika kuleta uwiano wa mwalimu, na wanafunzi
wa 1:60 ulioelekezwa;
i. Tunawaelekeza Wakuu wa Shule na Walimu
Wakuu kushirikiana na Bodi zao za shule ili
kufuata miongiozo ambayo Wizara imetoa kwa ajili
ya michango ya wanafunzi wanaoendelea na
masomo. Hatua kali zitachukuliwa kwa Mkuu wa
Shule au Mwalimu Mkuu yeyote ambaye ataenda
kuinyume na miongozo iliyotolewa na Serikali;
na
j. Walimu waliopo kazini na Waajiriwa wapya,
kuhakikisha wanafundisha wanafunzi kwa weledi,
na bidii ya hali ya juu kwa kuzingatia kalenda ya
ufundishaji iliyopo. Wakuu wa Shule, Waratibu
Elimu Kata, Maafisa Elimu wa Halmashauri na
Mikoa yote nchini kufuatilia ufundishaji wa kila
siku darasani, na kujiridhisha kuwa wanafunzi
wanapata umahiri unaotarajiwa kwenye ngazi
mbalimbali za elimu ya Msingi na Sekondari.
Aidha, Watumishi wote wa kada za Afya nchini,
wanaoendelea na utumishi, na walioajiriwa wapya,
kuhakikisha wanawahudumia wananchi kwa weledi na
upendo wa hali ya juu, kwa kuzingatia Sheria, kanuni
na miongozo ya utoaji bora wa huduma za afya nchini.
Ndugu Wanahabari
Majina ya waombaji wote waliopangiwa vituo vya kazi
yanapatikana katika Tovuti ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI
www.tamisemi.go.tz.
Asanteni kwa kunisikiliza.
Innocent L. Bashungwa (Mb.)
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI