EPISODE 18
ILIPOISHIA
“Unataka kuniambia bila kinga nisingeiona leo?”
“Hilo ni jibu uliza swali.”
“Kuhusu kwenda msibani itakuwaje?”
SASA ENDELEA
“Ukitaka nenda hawawezi kukufanya lolote.”
“Hatuwezi kutiana aibu kuwa mimi ndiye niliyemuua baba?”
“Wataanzia wapi, kwa kitendo walichokitenda jana usiku na leo kukuona hai wamezidi kuchanganyikiwa. Kama wangejua kama ni mimi ndiye niliyekukinga, basi wangenipa pesa nyingi ili wakupoteze.”
“Kuna umuhimu wa kuongeza kinga mwilini maana kama kinyonga kashindwa lazima wataendelea kutafuta kitu kingine,” nilijikuta nikijihami baada ya kuona vita iliyopo mbele na ndugu zangu ni nzito.
“Kijana kama kinyonga ameshindwa hakuna kitu chochote kitaweza japo kwa dawa yangu walikuwa wakijisumbua, uchawi ule ni mbaya sana.”
“Kwa hiyo unaniambiaje?”
“Ondoa wasiwasi, chochote kitakachokupata si mkono wa mtu bali amri ya Mungu.”
“Nashukuru mzee wangu.”
“Basi ondoa hofu hakuna chochote kitakachokukuta, kila atakayekugusa kitamrudia.”
Niliagana na mganga kisha nilimpitia mpenzi wangu na kurudi hotelini kujiandaa na kwenda msibani. Tukiwa njiani simu ya dada iliita, nilitaka kuacha kuipokea lakini niliipokea ili nijue ana shida gani.
“Haloo,” nilipokea.
“Asante Masalu, asante sana.. njoo umle nyama baba,” dada alisema kwa sauti iliyoonesha analia.
“Tena wewe ndiye ninayekutafuta mchawi mkubwa, nakuapia sitakusamehe wewe na wote hata marehemu baba mpaka nakufa. Vitendo vyote mlivyonitendea hamkuridhika mpaka mnaitaka roho yangu kwa nguvu? Hivi nikifa mtafaidika nini?”
“Nani anataka kukuua?”
“Kitendo mlichofanya wiki moja iliyopita sitawasamehe mpaka nakufa, mnanilaumu nahusika na kifo cha baba. Hebu niambieni mimi nimefanya nini kuchangia ugonjwa mpaka kifo cha baba. Kinyonga mliyemtumia ili mniue ndiye aliyemmaliza baba kwa taarifa yenu.”
“Ha! Umejuaje?” Dada alishtuka.
“Nakuapia nilikuwa nina mpango wa kuwasamehe, lakini kwa kitendo mlichokitenda jana saa sita usiku sitawasamehe milele na mimi nitajua cha kuwafanya, endeleeni kuroga nami sasa naingia vitani tuona nani zaidi.”
Kauli yangu ya vitisho japo sikuwa na nia hiyo ilimfanya dada akate simu.
“Masalu vipi mbona sikuelewi?” Mpenzi wangu aliniuliza.
“Wee waache tu.”
“Nani huyo?”
“Dada.”
“Mbona mnatishana?”
“Namtisha namwambia ukweli!”
“Kwa nini umewaambia mapema?”
“Lazima waujue ubaya wao na tena nawafuata msibani wanieleze kisa na mkasa cha kuyatafuta maisha yangu,” nilijikuta nikipandwa na hasira.
“Punguza hasira tukifika hotelini tutalizungumza, umeshawajua wabaya wako kwa nini usichanganyikiwe?”
Nilikubaliana na mpenzi wangu kurudi hotelini, tulipofika nilikuwa bado na hasira kwa kauli za dada kuwa nitamla nyama baba yangu aliyefariki kwa ajili yao wenyewe. Nilijikuta njia panda katika maamuzi yangu ya kwenda kwenye msiba wa baba. Nilijikuta nikipata ujasiri wa kwenda kwenye msiba wa baba.
“Aisee wacha niende kwenye msiba wa baba,” nilimwambia mpenzi wangu.
“Masalu nakuomba usiende.”
“Hapana lazima niende.”
“Panaweza kutokea ugomvi.”
“Na utokee, tena nakwenda kuwapa makavu.”
“ Nakuomba usiende mtatiana aibu.”
“Nisipokwenda watu hawatanielewa.”
“Bora wasikuelewe kuliko aibu itakayowakuta.”
“Hakuna aibu, mganga amesema hawatafunua midomo yao kusema lolote kwa kuiogopa aibu.”
“Mmh! Lakini ningekuwa mimi nisingeenda.”
“Lazima niende na leo watanitambua, siwezi kuishi na maadui zangu na kuwachekea.”
”Hayo ndiyo ninayokukataza, kama huwezi kuzuia hasira zako hakuna haja ya kwenda.”
“Nitajitahidi lakini moyo unaniuma baada ya kujua ubaya waliotaka kunifanyia usiku wa kuamkia leo.”
“Lakini si umepata kinga?”
“Ni kweli, lakini kama nisingepata ingekuwaje?”
“Ungepotea, lakini nakuomba ulimalize jambo hili kwa busara.”
“Nimekuelewa.”
Nilijiandaa na baadaye tuliondoka na mpenzi wangu ambaye nilimuacha nyumbani kwao na mimi kwenda kwetu. Nilipofika kulikuwa na watu wengi wamekusanyika nje ya nyumba yetu wakiwepo wafanyabiashara wenzetu.
Sehemu kubwa ilikuwa imejaa magari ya watu, nilipoteremka kwenye teksi na kutembea kwenda ndani, kila aliyenitazama alinishangaa. Wengi walinipa pole ya kifo cha baba, niliwaitikia na kuingia ndani. Nilipofika ndani ndugu zangu walishtuka kuniona.
Sikujali hali ile, niliingia chumba alichokuwa mama, aliponiona aliacha kulia na kunitazama kama kiumbe cha ajabu. Kwa vile kila kitu nilikuwa nakijua sikuijali hali ile na kumsalimia.
“Shikamoo mama.”
“Marahaba.”
“Poleni.”
“Asante.”
“Mnazika saa ngapi?”
“Sijajua mipango yote wanafanya ndugu zako.”
“Kwani Masalu ulikuwa wapi?” Mama wa jirani aliniuliza.
“Nilikuwa safari.”
“Ooh! Pole sana kwa kumpoteza kipenzi baba yako, najua kiasi gani alivyokuwa akikupenda.”
“Ni mapenzi ya Mungu.”
“Na kweli, ni yeye aliyetoa na ndiye aliyetwaa.”
“Kila neno litatimia.”
“Masalu,” sauti kali ya dada iliniita.
“Unasemaje?”
“Njoo nje.”
“Kufanya nini?”
“Nimekwambia njoo au nitakutoa kwa nguvu.”
“Jeuri hiyo huna.”
Je nini kiliendelea hapo msibani ? ..