Notification texts go here Contact Us Buy Now!

Baba Kiumbe Wa Ajabu sehemu ya 14

simulizi: BABA KIUMBE CHA AJABU
EPISODE 14
ILIPOISHIA
Siku ile tulishinda na kulala pale, majira ya saa tano za usiku dada alinipigia simu, nilitaka kuacha kuipokea lakini niliamua kuipokea.
HAYA SASA ENDELEA KUSISIMKA KIVYAKOVYAKO.
“Haloo.”
“Haloo Masalu.”
“Shikamoo”
“Marahaba.”
“Unasemaje?”
“Masalu upo wapi?”
“Una shinda gani?”
“Masalu umefanya nini?”
“Kuhusu nini?”
“Unataka kumuua baba?”
“Kumuua kivipi?”
“Masalu baba akifa utamla nyama.”
“Kama mlivyo mla nyama dada Monika?”
“Nini?”
“Umenisikia vizuri.”
“Wee fanya mzaha, lakini ole wako baba afe.”
“Na wewe ole wako siku ukisogeza pua yako kwangu utanitambua mimi ni nani mwanga mkubwa we, kwanza nilikuwa nakuchekea sasa hivi sikupendi nakuchukia ni adui yangu namba moja na taarifa zako nazipeleka polisi.”
“Polisi! Utawaambia nini?”
“Kwamba wewe na wenzako ni wauaji.”
“Tumemuua nani?”
“Dada Monika na mtoto wako na ushahidi wa sehemu ulipoziweka hizo maiti ninao na lazima mtanyongwa mwaka huu.”
“Masalu usifike huko hali ya baba ni mbaya sana, hebu rudi nyumbani tujue tufanye nini,” ilibidi arudishe sauti chini.
“Nirudi mnimalize.”
“Tukumalize?” Alijifanya kushtuka.
“Eeh, baada ya kuniua nguvu za kiume sasa mnataka kunigeuza msukule.”
“Ha! Masalu nani kakudanyanya hivyo?”
“Dada hakuna siri duniani, yaani pamoja na kunipa kidonda hamkuridhika pamoja na utajiri na maisha mazuri kupitia mwili wangu. Mkaamua kuniua nguvu za kiume ili nisiwe na thamani yoyote dunia. Haitoshi mmeniandalia pigo zito la kunimaliza kabisa la kunigeuza msukule ili tu muwe na maisha mazuri.
“Ninyi ni viumbe gani mnaojali fedha kuliko utu wa mtu, mmemtoa kafara dada Monika kwa tamaa zenu, hamkuridhika umemtoa mtoto wako ili uwe na pesa nyingi vile vile hamkuridhika mmenigeukia mimi. Kwa vile hakuna mtu mwingine wa kumpa kidonda hiki mmeamua mnigeuze ndondocha wa familia.”
“Masalu umejuaje?”
“Si kujuaje, kwa nini umeamua kunifanya hivyo?”
“Si kweli,” dada alijifanya kushtuka.
“Sawa si kweli, basi baba anakufa.”
“Umeamua kuuana?”
“Masalu bila wewe baba atakufa, unakubali baba yetu afe kweli?”
“Mimi na ninyi nani kaamua kumuua mwenzake?”
“Masalu kumbuka baba yetu ni huyuhuyu, akifa hatutampata mwingine.”
“Kwani kuna mbadala wa dada Monika, baba ni huyo huyo, dada Monika mwingine yupo wapi?”
“Masalu makosa yamekwisha fanyika rudisha moyo uokoe maisha ya baba.”
“Kwanza mnaniambia hivyo mimi nimemfanya nini baba?” niliwauliza swali gumu.
“Inaonekana umekwenda kwa mganga kurudisha nguvu zako za kiume.”
“Mlitaka niwe hivihivi milele kwa raha zenu, mbona ninyi mna watoto na wanaume?”
“Kwani Masalu upo wapi?”
“Tokea lini mlinitafuta?”
“Basi zungumza na mama,” baada ya muda nilimsikia mama akiniita.
“Masalu.”
“Naam mama, shikamoo.”
“Marahaba mwanangu upo wapi? hali ya baba yako ni mbaya sana.”
“Anaumwa nini?”
“Ameanguka kwenye mishughuliko yake, kama ni kweli umefanya wewe njoo umsaidie baba yako, hali inatisha hajitambui anakoroma tu.”
“Mama sihusiani na lolote kuhusiana na matatizo ya baba, naomba mumpeleke hospitali.”
“Ugonjwa huu si wa hospitali.”
“Kwa hiyo mimi ndiye niliyemroga?”
“Hapana Masalu, ila inawezekana ulichokifanya ndicho kilichomuathiri baba yako.”
“Kipi hicho?”
“Unakijua Masalu, hebu rudi haraka nyumbani.”
“Mama ni nani kwako?”
“Mtoto.”
“Nina haki gani kama mmoja wa watoto wako?”
“Haki zote kama walizonazo wenzako.”
“Sasa kama kila mtu ana haki hiyo kwa nini unataka kushiriki katika kunigeuza ndondocha wa familia?”
“Masalu! Wakugeuze kivipi?” mama alishtuka.
“Mama, unajua vizuri sana si suala la siri, mpango wenu wa kunimaliza nimeugundua lakini nawahakikishia kila atakayenigusa nitampoteza.”
“Upo tayari baba yako afe?”
“Mimi situnzi uhai wake bali Mungu aliyetuumba wote, kama wakati wake umefika basi atakufa, kama alivyokufa mtoto wa dada na dada Monika.”
“Kwa nini umekosa huruma?”
“Kwa vile ninyi mnanionea huruma eeeh.”
“Kama ulivyosikia hali ya baba yako ni mbaya kifo chake kitakuhusu.”
“Sishangai hata wewe mama niliyekuwa nakutegemea ni mmoja wapo. Asante sana nashukuru, Mungu yupo atanilinda.”
“Masalu...Masa..,” nilikata simu na kuizima kabisa.
******
Baada ya mazungumzo nilijikuta nikilia peke yangu jinsi familia yangu ilivyokuwa ikijijali yenyewe na kuwa tayari kupoteza uhai wa mtu ili tu ipate mali.
“Masalu nyamaza mpenzi wangu,” mpenzi wangu alinibembeleza, kipindi kile yeye ndiye aliyekuwa mfariji wangu.
“Inaniuma.”
“Kweli inauma, lakini kwa nini umekubali kuzungumza nao? Ungezima simu yote haya yasingetokea.”
“Ilikuwa lazima nizungumze nao ili wajue kuwa naelewa kila kitu, pia hata kujua kama kweli hali ya baba ikoje.”
“Kwa hiyo utakwenda kumuona baba yako?”
“Nikitoka kwa mganga nitakwenda.”
“Pole sana inasikitisha, familia yako ina dhambi kubwa.”
“Wee waache sijui kwa Mungu watasema nini?”
“Ulisema wewe ndiye chanzo cha utajiri kilichoachwa na marehemu dada yako Monika, ukipona itakuwaje?”
“Sijui, watajua wenyewe, mimi nitaangalia afya yangu.”
“Mmh! Pole sana mpenzi wangu, kupona lazima uwe na roho ngumu ili umeze mfupa.”
“Nimekwisha umeza lolote na liwe, siwapendi mashetani wale.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda tulipanda kitandani kulala, usiku nilijikuta nikipatwa na hamu ya mapenzi. Lakini nilikumbuka kauli ya mganga kuwa nikikutana kimwili na mwenzangu ndiyo kifo cha baba, hawezi kuomba hata maji.
Pamoja na hasira kutokana na roho mbaya ya familia yangu juu ya mambo waliyotaka kunifanyia nilijikuta nikiingiwa na imani ya kutofanya tendo lile kuokoa maisha ya baba. Tulilala mpaka asubuhi bila kufanya tendo la ndoa, asubuhi tuliamkia kwa mganga.
Hatukuchelewa kufika kwa vile hapakuwa mbali kutoka tulipokuwa tumepanga, ulikuwa mwendo wa dakika ishrini. Ilionesha sisi ndiyo tulikuwa wateja wa kwanza toka nje kufika pale kwa siku ile, tuliowakuta pale ni wale waliokuwa wakitibiwa na kulala palepale.
Mganga alitukaribisha, kama kawaida niliingia ndani peke yangu na mpenzi wangu alibakia nje. Nilipofika hakunisemesha lolote, aliendelea na kutoa chupa za dawa kwenye kikapu na kuziweka juu ya ngozi kisha alichukua karatasi ya kaki na kuanza kumiminia unga wa dawa kidogo kidogo kutoka katika kila chupa.
Zilikuwa chupa zaidi ya tano, baada ya kuukusanya unga wa dawa katika karatasi moja, alichukua chupa iliyokuwa na mafuta kama sikosei ya ng’ombe, yalikuwa meupe na mazito. Aliyamiminia yale mafuta na kuyachanganya na mchanganyiko wa dawa kisha alitoka nje.
Baada ya muda alirudi na kunionesha kwa ishara nimfuate, nilimfuata mpaka kwenye kichuguu kimoja ambacho alinielekeza. Kabla ya kupanda juu ya kichuguu alinielekeza kwa ishara nivue shati. Nami nilifanya kama alivyonielekeza.
Baada ya kupanda juu ya kichuguu kifua wazi, alipanda na yeye na kuanza kunichanja kila kona ya mwili huku akinipaka ile dawa aliyochanganya na mafuta mazito. Alipomaliza tuliteremka na kurudi hadi ndani ya kilinge, ndipo aliponisemesha.
”Habari za toka jana?”
“Nzuri mzee wangu, shikamoo.”
“Marahaba, kuna habari gani mpya?”
“Jana walinipigia simu usiku na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”
“Uliwajibu nini?”
“Niliwaambia siwezi kujiteketeza mwenyewe.”
“Wao walisemaje?”
“Walinitishia kama baba akifa nitamla nyama.”
“Akawajibu nini?”
“Niliwaeleza kama walivyokula nyama ya dada Monika.”
“Wakasemaje?”
“Walishtuka na kunieleza kuwa habari nimezijulia wapi?”
“Mh, ukawajibu nini?”
“Niliwambia nitawapeleka polisi na kuwafungulia mashtaka ya uuaji na kukaa na maiti za watu ndani?”
“Enhee! Wakasemaje?”
“Walishtuka na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”
“Ukawajibu nini?”
“Niliwaeleza sipo tayari.”
”Wakasemaje?”
“Waliendelea kunibembeleza niende kwa vile uliniahidi nikitoka hapa nitakuwa kamili, nimewaeleza nitakwenda leo.”
“Wakasemaje?”
“Tumekubaliana, nikitoka hapa niende.”
“Sikiliza, una bahati kama usingekuja hapa na kujipendekeza jana ukaenda ungekwisha palepale.”
“He!” Nilishtuka kusikia vile.
“Unashtuka, kama nilivyokueleza familia yako haina mapenzi na wewe kwa ajili ya mali.”
“Mmh! Sasa nikienda leo itakuwaje?”
“Leo usiende, nenda keshokutwa ila kuna kitu kitatokea si cha kawaida, kuwa tayari kukabiliana nacho.”
“Kitu gani hicho?”
“Wee nenda, ila majibu utayapata kujua kinga niliyokukinga inafanya kazi kiasi gani.”
“Niambie ili nijue ikiwezekana nisiende.”
“Lazima uende ili kuwaumbua wabaya wako.”
“Mmh! Sawa.”
“Baada ya kesho kwenda rudi tumalizie tiba, kwa vile hawatakubali kuona umewashinda.”
“Sawa nimekuelewa.”
“Nilitaka kusahau kitu kimoja, leo usioge wala kukutana na mwanamke kimwili ikiwezekana leo kila mmoja alale chumba chake au kitanda chake.”
“Sawa nimekuelewa.”
“Ndoto utakayoiota ndilo jibu la safari yako.”
“Nashukuru kwa msaada wako.”
Je nini kitatokea. ?

About the Author

Hello,I am Web Designer and Expert facebooktwitteryoutubeinstagramexternal-link

Chapisha Maoni

Cookie Consent
We serve cookies on this site to analyze traffic, remember your preferences, and optimize your experience.
Oops!
It seems there is something wrong with your internet connection. Please connect to the internet and start browsing again.
AdBlock Detected!
We have detected that you are using adblocking plugin in your browser.
The revenue we earn by the advertisements is used to manage this website, we request you to whitelist our website in your adblocking plugin.
Site is Blocked
Sorry! This site is not available in your country.