Notification texts go here Contact Us Buy Now!

Baba Kiumbe Wa Ajabu sehemu ya 13

simulizi: BABA KIUMBE CHA AJABU
EPISODE 13
ILIPOISHIA
“Sikiliza kijana usijitoe akili, kwa jinsi alivyokuelekeza dada yako mkubwa juu ya kupona nguvu zako za kiume, nini kitampata baba yako?”
“Kwa hiyo nibaki na hali hii milele?”
“Ni uamuzi wako, kupona upoteze watu au uendelee kuwa maiti inayotembea ili kuiokoa familia yako. Na hiyo mosi familia yako sasa hivi itakutuliza ndani kwa kupooza miguu, utakuwa wa kula na kulala wao wanaponda maisha.”
“Eti?”
SASA ENDELEA NAYO KIVYAKOVYAKO.
“Ukweli ndiyo huo mpango huo utatekelezwa mara moja baada ya kuonekana umekuwa mkaidi.”
“Sikubali.”
“Kama hukubali utafanya nini?”
”Nitatibiwa kila kitu nihakikishe napona na litakalowatokea watajijua wenyewe.”
“Usiseme kwa hasira, upo tayari kuisambaratisha familia yako?”
“Nipo tayari.”
“Kwa kukupa mfano mdogo, dawa utakayokunywa itarudisha nguvu zako za kiume, lakini ukirudi nyumbani utamkuta baba yako yupo hoi kitandani.”
“Kitakachofuata?”
“Siku ukifanya mapenzi ndiyo siku ya kifo chake.”
“Mmh!” Niliguna.
“Ukweli ndiyo huo, chagua kusuka ama kunyoa?”
Nilibakia kimya kwa muda nikiwaza nitakachokifanya na matatizo ambayo yangeikuta familia yangu. Nilikuwa radhi kuendelea na kidonda changu na kukosa nguvu za kiume. Lakini maelezo ya mganga kuwa wanataka kunigeuza msukule kwa ajili ya kuendeleza mali kilinichanganya sana.
Kufikia pale nilijikuta nikichanganyikiwa na kushindwa niegemee upande gani, lakini niliamini maisha yangu ni muhimu kuliko kitu chochote chini ya jua. Vilevile sikuwa tayari kumhurumia mtu aliyepanga kuniangamiza kwa ajili ya tamaa zake za mali.
Uamuzi nilioamua ni kujitengeneza mimi na lolote litakalotokea kila mmoja ataubeba msalaba wake.
Baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu mganga alinishtua.
“Vipi umeamua nini maana naona umekaa kimya?”
“Mzee wangu mambo ni mazito kila ninalofikiria naliona zito.”
“Kwa hiyo tuache kama ilivyo?”
“Mzee wangu huna ufumbuzi mwingine usio na madhara?”
“Sikiliza kijana wewe unajua matatizo ya familia yenu kuliko mimi, hebu nisaidie nifanye nini?”
“Wewe si ndiye mtaalamu ninayekutegemea?”
“Hutaki kunisikiliza, kwani mimi napenda kuona matatizo, lakini mambo yenyewe yamekaa vibaya.”
“Kwa hiyo?”
“Nimekueleza yote una uamuzi wako mwenyewe wala siwezi kukuingilia lakini ukweli ndiyo huo.”
“Basi fanya unavyoweza.”
“Vipi?”
“Utakaloliona linafaa.”
“Kijana acha kujitoa akili, mimi sipo hapa kwa ajili ya kuwachagulia wateja jinsi ya kufanya.”
“Mzee wangu kwa vile mpango wao ni mbaya kwangu naomba unisaidie mimi.”
“Kwa hiyo upo tayari kwa lolote litakalotokea?”
“Nipo tayari.”
Leo nitaanza kukupa dawa ya kurudisha nguvu za kiume, lakini usishtuke kusikia taarifa zitakazokufikia ambazo zitajenga uadui mkubwa kati yako na nduguzo.”
“Siwezi kushtuka kwa viumbe wasio na huruma na mimi, wewe nipe hiyo dawa kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.”
“Haya nisubiri.”
Mganga alinyanyuka na kutoka nje, akiniacha na uamuzi mmoja ambao nilikuwa tayari kwa lolote. Baada ya muda aliniita nje, nilitoka na kuelezwa nisubiri kwenye kigoda. Baada ya muda nilimuona mpenzi wangu akiwa amebeba ndoo kutoka kwenye kisima kilichokuwa pembeni ya nyumba ya mganga.
Alipofika, mganga alimueleza ayapeleke nyuma ya nyumba na kuyaweka kwenye beseni. Alifanya vile, aliporudi mganga alizunguka nyuma na baada ya muda aliniita. Nilimfuata na kukuta kuna beseni lililokuwa na maji yaliyochanganywa na dawa ya unga na majani mabichi kama ya mnyonyo.
“Oga haya maji, kisha haya majani utajisugua sehemu zako zisizofanya kazi, sawa?”
“Sawa.”
“Haya, ukimaliza kuoga vitu vyote viache hukuhuku.”
“Hakuna tatizo mzee.”
Mganga aliondoka na kuniacha nikivua nguo na kuanza kujimwagia maji kwa mikono huku nikijisugua kwa majani yale mabichi sehemu zangu za siri zilizokwisha nguvu. Baada ya kumaliza kuoga nilirudi kwa mganga, alinielekeza nikae kwenye kigoda kisha alizunguka nyuma ya nyumba, sikujua anakwenda kufanya nini, mara alirudi akiwa ameshikilia majani niliyojisugulia na kuingia kwenye kilinge chake. Baada ya muda aliniita.
Niliingia kibandani na kuketi kwenye ngozi ya ng’ombe, baada ya kuketi mganga alinipa maji yaliyokuwa kwenye kikombe cha plastiki. Nilikunywa maji yale kisha nilimrudishia kikombe, baada ya kukipokea alisema:
“Sasa nafikiri kazi tumemaliza, weka hapo kwenye kikapu kiasi chochote kama sadaka kwa mizimu.”
Nilichomoa pochi na kuweka elfu hamsini, baada ya kuweka mganga alisema:
“Mpaka sasa kwenu kuna hali ya sintofahamu, inaonesha hapa baba yako ameanguka dukani na anarudishwa nyumba. Ukitaka kumuua haraka baba yako ukikutana na mpenzi wako haimkopeshi, salamu utasikia.”
“Sasa mganga kama ni hivyo kuna faida gani ya kuja kwako?”
“Nilikuwa nakujulisha tu, litakalotokea usishangae, kesho asubuhi njoo haraka maana kuna vita nzito itakayotokea. Itakuwa mara mbili ya leo, ningeweza kukutengenezea zindiko lakini siwezi kufanya kazi mbili kubwa kwa wakati mmoja.”
“Hakuna tatizo.”
“Basi wewe nenda nyumbani, kama unaweza usionane nao watakutafuta sana ili kuhakikisha baba yenu anarudi katika hali ya kawaida. Na kurudi kwa afya ya baba yako, huchukui muda unakuwa msukule wa familia wa kuwaingizia pesa.”
“Siwezi kukubali, kama nimepona nitaendelea na mpenzi wangu kwa vile bila yeye nisingeweza kupona.”
“Pia kuna kitu cha ajabu kitamtokea baba yake, sumu ya uchawi itamgeuza kiumbe cha kutisha.”
“Vyovyote atakavyokuwa mimi hainihusu, yule sasa ni adui yangu na si mzazi wangu,” pamoja na maneno yale kuwa ya kutisha sikuingiwa huruma kwa vile wao walitafuta uhai wangu.
“Hiyo ni juu yako kwa vile yote nimekueleza bila kuacha kitu.”
*****
Baada ya maelezo ya mganga, nilitoka na kumpitia mpenzi wangu na kuondoka, tulipofika Pasiansi tulitafuta sehemu kupata chakula kutokana na njaa iliyokuwa ikituchonyota.
Wakati wa kula nilijikuta mtu mwenye mawazo mengi, kitu kilichomshtua mpenzi wangu na kutaka kujua kulikoni.
“Masalu kuna nini mbona unaoneka una mawazo mengi?”
“Ni kweli, nina mtihani mzito.”
“Upi huo?”
“Kuhusiana na hali yangu, kama nilivyokueleza, kuna mambo mazito yamejitokeza.”
Sikuwa na jinsi nilimueleza kila kitu, sikutaka kumficha kwa vile msaada wake ndiyo uliofichua yote. Baada ya kunisikiliza alishtuka sana.
“He!”
“Ndiyo hivyo nikubali ili nigeuzwe ndondocha au niokoe maisha ya baba na familia kukutwa na matatizo mazito.”
“Mmh! Huo mtihani, lakini maisha yako ni muhimu kuliko kitu chochote.”
“Nami ndiyo nimefanya hivyo, ila mganga ameniomba leo nisionane nao ili kesho turudi mapema kwake.”
“Hakuna haja ya kuhangaika, tutafute gesti yoyote nzuri hapahapa Pasiansi ili kesho turudi kwa mganga mapema.”
“Kweli wazo zuri, basi tufanye hivyo.”
Nilikubaliana na mpenzi, wangu baada ya chakula tulitafuta nyumba ya wageni yenye hadhi na kupanga pale.
Siku ile tulishinda na kulala pale, majira ya saa tano za usiku dada alinipigia simu, nilitaka kuacha kuipokea lakini niliamua kuipokea.
Je nini kitaendelea?

About the Author

Hello,I am Web Designer and Expert facebooktwitteryoutubeinstagramexternal-link

إرسال تعليق

Cookie Consent
We serve cookies on this site to analyze traffic, remember your preferences, and optimize your experience.
Oops!
It seems there is something wrong with your internet connection. Please connect to the internet and start browsing again.
AdBlock Detected!
We have detected that you are using adblocking plugin in your browser.
The revenue we earn by the advertisements is used to manage this website, we request you to whitelist our website in your adblocking plugin.
Site is Blocked
Sorry! This site is not available in your country.