MOYO ULIOJAA MAUMIVU
SEHEMU YA 29
Mara baada ya kujua kwamba Violeth alikuwa na mimba, makampuni mbalimbali yakaanza kujisogeza na kuomba kufanya nao biashara, yaani mtoto atakapozaliwa basi wao wawe wa kwanza kumpiga picha na kumtupia kwenye mitandao ya kijamii.
Lilikuwa dili kubwa sana. Benki kubwa ya Africa Union ikapanga kuingiza kiasi cha shilingi milioni mia nne kwa umiliki wa picha ya kwanza kwa mtoto atakayezaliwa.
“Ila watakuwa mapacha,” alisema Theo huku akimwangalia meneja wa benki hiyo.
“Mapacha?”
“Ndiyo!”
“Basi tutaweka mara mbili zaidi. Naomba asichukue mtu nafasi hiyo,” alisema meneja huyo.
“Haina shida.”
Mimba yake ilikuwa ni ya mwezi mmoja lakini kila alipopita watu walikuwa bize kuangalia tumbo lake. Alionekana kuwa mwanamke mwenye furaha mno, alitabasamu kila wakati, mapenzi yao yalikuwa wazi na hawakutaka kujificha hata kidogo.
Theo alisimamisha mambo yake mengine kwa ajili ya mke wake, aliamini huyo ndiye alikuwa furaha yake, bila yeye maisha yake hayakuwa na kitu hivyo ilikuwa ni lazima amuheshimu kwa kila kitu.
Siku zilikwenda mbele, miezi ikakatika mpaka ulipofika mwezi wa mwisho, mwezi wa uchungu ambao alitakiwa kwenda kujifungua. Mwezi huo waandishi wa habari walikuwa makini, masikio yao yalikuwa ni kusikilizia ni hospitali gani Violeth angekwenda kujifungulia.
Hakukuwa na aliyejua, Theo hakumwambia mtu yeyote yule, alifanya kila kitu kuwa siri. Kazi ilikuwa kwa Watanzania, wazee wa kubashiri, wengine walisema Violeth angejifungulia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, wengine walisema Agha Khan, wengine Hindu Mandal, kila mtu muda huo alisema lake.
Theo alitafutwa ili alizungumzie jambo hilo, hakutaka kusema lolote lile, aliwaambia waandishi kwamba walitakiwa kusubiri kwani huo haukuwa muda sahihi wa kuwaambia kitu chochote kuhusu mke wake.
Siku zilikatika mpaka siku ambayo Violeth alijisikia uchungu na kupelekwa katika Hospitali ya kisasa ya St. Joseph Medical Centre iliyokuwa Upanga kwa ajili ya kujifungua.