Notification texts go here Contact Us Buy Now!

FIKIRIA UTAJIRI

FIKIRIA UTAJIRI ILI ufanikiwe unatakiwa kutumia uwezo na nguvu ambazo tayari unazo. Inakubidi kuwa mshindani, kukubali kuwa unaweza na kufanya bidii zaidi. Pia yakupasa uwe na utayari wa kutaka kuwa na mafanikio katika maisha yako. Pasipokuwa na utayari hutafanya chochote. Vyoyote vile utakavyofikiri kuwa tajiri katika akili yako utafanikiwa. Tuangalie mfano wa kweli uliomtokea mkulima mmoja maskini aliyekuwa anai
Estimated read time: 35 min

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 01

ILI ufanikiwe unatakiwa kutumia uwezo na nguvu ambazo tayari unazo. Inakubidi kuwa mshindani, kukubali kuwa unaweza na kufanya bidii zaidi.
Pia yakupasa uwe na utayari wa kutaka kuwa na mafanikio katika maisha yako. Pasipokuwa na utayari hutafanya chochote.
Vyoyote vile utakavyofikiri kuwa tajiri katika akili yako utafanikiwa.
Tuangalie mfano wa kweli uliomtokea mkulima mmoja maskini aliyekuwa anaishi katika Bara la Afrika, ambaye alikuwa na shamba kubwa la dhahabu bila yeye kujua. Mkulima huyo alitumia muda na miaka mingi akijitahidi kupanda mazao katika shamba lake ambalo lilikuwa gumu kulilima na lenye miamba.
Kutokana na ugumu aliokuwa anakabiliana nao, mkulima huyo alipumbazwa na utajiri wa haraka haraka ambao angeupata kutoka kwa mtu mmoja ambaye alikuwa anatafuta madini ya dhahabu katika maeneo mbalimbali kwa kufanya utafiti. Kwani naye mtu huyo alikuwa anataka kuwa tajiri.
Mkulima yule kwa kuwa alichoka kulima, aliamua kuuza shamba lake kwa mtu yule aliyekuwa anatafuta madini ya dhahabu. Alipata pesa akawa na maisha mazuri kwa muda, mwishoni alikata tamaa, aliishiwa fedha, alivunjika moyo na kupata hisia za kujirusha mtoni ambapo alizama na kufariki dunia.
Wakati huo, mtu yule aliyenunua shamba la mkulima wakati akifanya utafiti wake alikuta jiwe lisilo la kawaida katika mto uliopita katika shamba lake.
Alilipima na kukuta ni jiwe kubwa la dhahabu lenye thamani. Hivyo tangu wakati huo mtu huyo alikuwa ni mojawapo kati ya matajiri wakubwa duniani.
Yakupasa katika maisha yako ya kila siku kutokuchukua maamuzi ambayo baadaye yataleta hasara katika maisha yako au familia yako kwa ujumla.
Unapokuwa na kitu kabla hujachukua hatua yoyote ya kukiuza au kubadili uamuzi wako wa awali juu ya kitu hicho ni vizuri kuomba ushauri kwa watu unaowaamini na kuwategemea.
Si wote watakaokushauri vizuri, ni juu yako wewe kuweza kupima ni ushauri gani ambao unaweza ukakufaa kutokana na mwelekeo wa jambo lako.
Tukirudi katika mfano wetu tunaona kwamba, mkulima wa kwanza hakujua kuwa alikuwa anamiliki shamba kubwa lenye madini ya dhahabu.
Kama angeomba ushauri au angepoteza muda wake kufanya utafiti katika shamba lake, naye angekuwa ni mmoja kati ya matajiri waliopo.
Alilima, alichoka akaamua kuuza mali yake kwa ajili ya kutafuta bahati yake katika shughuli nyingine bila kugundua kuwa shamba alilokuwa nalo ndio utajiri wake.
Angejaribu kuchunguza kwa nini hilo shamba lake lina miamba mingi na anaweza kunufaikaje nalo, asingefikia hatua ya kujirusha mtoni na hatimaye kufariki dunia.
Mfano huu unamhusu kila mmoja wetu ambaye anafananishwa kuwa na shamba lenye madini ya dhahabu. Kwa maneno mengine kila mtu katika kazi yake anayoifanya iwe ni kilimo, biashara, uvuvi nk, kama atatulia na kuifanyia tathmini kazi yake na kuamua kupiga hatua zaidi lazima atafanikiwa.
Usiwe mwepesi wa kuachilia mambo kutokana na ugumu wake na kufikia hatua ya kukata tamaa, kuvunjika moyo na hata wengine kuchukua uamuzi wa kujiua. Kama kila mtu atatulia na kufanya utafiti katika shughuli yake anayoifanya atagundua kuwa ana utajiri mwingi, haijalishi kama ni utajiri wa malighafi, roho au vyote.
Kabla hatujaanza kukimbia huku na kule kufikiria kutafuta shamba lenye majani mabichi, tuhakikishe kuwa mashamba tuliyonayo tunayatumia vizuri. Mara nyingi, tunapoendelea kuangalia mashamba mengine, watu wengine nao wanaangalia mashamba yetu.
Kumbuka maandalizi yanakufanya kumaanisha jambo lolote unalotaka kulifanya, kwa kuwa utakuwa umelifanyia tathmini.
Mtafiti mmoja aliwauliza watu 3,000 kila mmoja peke yake kuwa wanaishi ili iweje? Mtafiti huyo alipatwa na mshtuko alipogundua kuwa asilimia 94 ya watu wote walioulizwa hawakuwa na sababu za msingi. Hao walikuwa ni wanawake na wanaume ambao wamekuwa wakipata taabu na kuendelea kuvumilia wakati wanasubiri siku nyingine mpya ianze katika maisha yao.
Mtafiti huyo aligundua kuwa watu hao walikuwa wakisubiri jambo fulani liweze kutokea ili maisha yao yabadilike, walikuwa wakisubiri siku ya kesho, wakisubiri mwaka ujao, wakisubiri watoto wao wakue na waondoke nyumbani pia fulani afariki ndipo waanze kuchukua hatua ya kufanya jambo kubwa la kubadilisha maisha yao.
Hii haileti maana wakati unapozungumzia kumwondoa mtu katika hali aliyonayo na kuwa katika hali bora zaidi.
Kumbuka jana imepita, na kesho hujui kama utakuwepo. Mtu yeyote ambaye hana malengo anaishi maisha ya kubahatisha. Ni vizuri kufahamu sheria ambazo zinaweza kukuongoza katika maisha yako ya kila siku. Dunia ni yako kama utaijua siri ya mafanikio.
Wakati mwingine vitu tulivyonavyo kama nyumba, gari au vinginevyo vinaweza kuharibika kabisa lakini upo uwezekano wa kupata vingine kama utakuwa na malengo ya kuwa na mafanikio zaidi ya hapo ulipokuwa. Jambo la msingi usikate tamaa.
Mtu yeyote anaweza akapitia kipindi kigumu cha kuishiwa na kufilisika kabisa, lakini inawezekana kupata bahati nyingine ya kutajirika. Hali hiyo inaweza kutokea mara kwa mara lakini cha msingi fanya bidii bila kukata tama, ukijua kuwa unapambana na maisha.
Hata kama umepata janga la kuunguliwa na nyumba yako, upo uwezekano wa kuijenga tena.
Kwa hiyo tumepata bahati kwa kuwa na nguvu isiyozuilika ya kufanya jambo kila unaponuia kufanya hivyo.
Maisha ya utajiri yanamzunguka kila mmoja wetu, inatakiwa upokee maisha hayo kwa moyo wa ukunjufu.
Fikiri kwa muda. Kufikiri ni zawadi kubwa ambayo inakupa matarajio kwa mambo yako yajayo ambayo umeyapanga.
Gari unaloliendesha, nyumba unayoishi, kiti unachopumzikia, vyote hivyo ulivipata baada ya kufikiri.
Ni kwa nini watu wengi wanaendelea kushindwa katika maisha yao? Ni kwa sababu watu wengi hawajui kanuni mbalimbali za maisha wanayoyaishi. Kwa kushindwa kuelekeza fikra zao katika mambo wanayoyatarajia.
Umekuwa ukiruhusu mawazo yako kuwa kizuizi cha mafanikio yako? Kwa kuwa na mawazo hasi, mawazo ya umaskini, ukabila, wasiwasi au uwoga? Kama ndivyo, badilika. Chukua muda kila siku kufikiria, kuchuja na umakini katika mipango yako unayoipanga.
Utaona kuwa fikra zako zina nguvu pamoja na kukua. Kila unapoendelea kufikiria, ndipo mipango yako inapoimarika. Baadaye, utafanikiwa na kuwa mtu mwenye maendeleo.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 02

UMEKUWA ukiruhusu mawazo yako kuwa kizuizi cha mafanikio yako? Kwa kuwa na mawazo hasi, mawazo ya umaskini, ukabila, wasiwasi au woga? Kama ndivyo, badilika. Chukua muda kila siku kufikiria, kuchuja na umakini katika mipango yako unayoipanga. Utaona kuwa fikra zako zina nguvu pamoja na kukua. Kila unapoendelea kufikiria, ndipo mipango yako inapoimarika. Baadaye, utafanikiwa na kuwa mtu mwenye maendeleo.
Kumbuka mawazo ndiyo mwanzo wa mafanikio yako. Unapokuwa na ndoto ya mafanikio kwanza yakupasa kuwa na wazo lako ambalo baadaye unatakiwa kulifanyia kazi, ili utengeneze bahati yako. Kwa kufuata maelekezo hayo utakuza upeo wako.
Ota ndoto kubwa. Wengi wanaweza kukupotosha kutokana na utajiri wa malighafi ulionao na kukudanganya kwa njia nyingi, lakini hakuna mtu anayeweza kukupotosha katika msimamo na kutumia fikra zako.
Wengi wanaweza wasikutendee haki, kama wengi wafanyavyo, wanaweza kukupotosha katika uhuru ulionao, lakini hawawezi kukuchukulia mawazo unayoyawaza. Kutokana na fikra zako utakuwa unashinda siku zote. Unataka kuwa na furaha? Unataka kuwa na amani? Unataka kuwa na cheo, nguvu au utajiri? Fikiri kuwa navyo, utafanikiwa.
Fikra unazowaza ni muhimu kuliko ujuzi ulionao. Ujuzi una mipaka, mawazo yanatawala muda wote, yanaleta maendeleo. Kila mtu binafsi anakuwa na ndoto za mafanikio bila kujitambua. Kwa mfano, wazazi wanapopanga ni jinsi gani watawaendeleza watoto wao, wajasiriamali wanapopanga ni jinsi gani wataendeleza biashara zao hiyo yote ni mifano ya kuwa na ndoto njema ya mafanikio.
Watu wachache wamejifunza kutumia mawazo yao kwa faida lakini wengi wetu mawazo tuliyonayo yanapata kutu kutokana na kutoyafanyia kazi. Hakuna sababu ya kuona aibu katika dunia ya ubunifu.
Kuwa na mawazo ya kufanya jambo fulani ni kitu kizuri katika dunia hii tunayoishi. Kila mmoja wetu ana kiwanda chake cha kuwa na mawazo. Lakini ni wapi mawazo hayo yanapotoka? Ni wapi waandishi, wana sayansi na wabunifu wanapopata mawazo makubwa? Kwa nini baadhi ya watu wengine wanakuwa wabunifu zaidi ya wengine? Ni kutokana na kutumia vizuri mawazo yao.
Kila mmoja wetu, kwa wakati mmoja au mwingine, lazima kujifunza chanzo halisi cha mawazo. Utajiri, unaweza kuupata, inategemeana na ulivyoyaweka mawazo yako. Wazo dogo rahisi linaweza likabadilisha kabisa maisha yako uliyonayo. Pia huwezi ukajua ukubwa wa mafanikio yako mpaka utakapojifunza jinsi ya kuchanganya juhudi zako na mawazo yako. Kwa vyovyote unapotaka mafanikio unajitathmini wewe mwenyewe.
Mwili uliopumzika una nguvu, vile vile akili. Kama unataka kuwa mbunifu na mpokeaji wa mawazo mapya, inakubidi kupata muda kwa mawazo hayo na kuyafanyia kazi.
Jizoeze kila siku kuwa na muda wa mapumziko, chagua chumba kizuri kilichotulia au kiti kizuri ambacho kitakusaidia kutuliza akili kwa urahisi. Unavyoendelea kujifunza kupumzika, utapata mawazo ambayo yatakufikisha katika malengo na matarajio yako.
Mtunzi anafikiri juu ya uimbaji, mchoraji anafikiri juu ya rangi, mwandishi anafikiri juu ya habari na maneno. Kama utachukua wazo moja na kulitendea kazi litakupa matokeo mazuri. Yafanyie kazi mawazo yanayokujia. Kuwa na utayari katika kunasa mawazo yako. Mawazo mengi mazuri yanapotea kwa sababu hayawekwi kwa maandishi.
Tathmini mawazo yako. Mara tu unapomaliza kuyachuja mawazo yako, unachagua yale unayotaka kuyafanyia kazi. Utagundua kuwa nayo yanahitaji kuongezewa ubora wake. Jifunze kutokufunga milango yako ya kuwa mbunifu.
Ni jambo lisilowezekana kati yetu kuwa kinyume na ujuzi tulionao. Mfano mtu hawezi kupita mbele ya gari liendalo kasi kwa kuwa anajua kuwa ataumia, hawezi kuogelea baharini kama anajua kuwa atazama, hawezi kuwa mstari wa mbele katika jambo la hatari kama anajua kuwa atadhurika.
Mafanikio hayahitaji kuwa na kiasi kikubwa cha ujuzi juu ya jambo fulani, lakini unatakiwa kung’ang’ania ili uweze kupata mafanikio hayo kwa ujuzi wowote ulionao.
Mkulima mmoja aliyejulikana kwa jina la Walter na ambaye siku za usoni angependa kuwa mchezaji bora wa mpira wa miguu, alimuuliza rafiki yake kuwa amewezaje kupata sh milioni 10 katika kazi yake anayoifanya kutokana na ujuzi alionao na kuweza kushinda kila dhana ya kushindwa ambayo ilikuwa inaibuka katika utendaji wake?
Rafiki huyo alimjibu kuwa wakati anaanza, alijua anataka kufanya nini na anachotarajia kukipata. Alikuwa na njozi iliyomwezesha kujenga picha katika mawazo yake kulingana na malengo aliyotaka kuyafikia katika maisha yake. Hivyo hiyo ndiyo siri kubwa ya mafanikio katika maisha yake.
Walter alisema kuwa kuna wakati alisikia umati wa watu ukishangilia katika mawazo yake. Kuna wakati alijenga picha ya sherehe ya kupewa tuzo iliyojaa waandishi wa habari za michezo, wageni na wanamitindo mbalimbali. Ndoto hiyo sasa ameanza kuifanyia kazi, hivyo anaamini atafanikiwa kama rafiki yake huyo alivyofanikiwa.
Inaonyesha watu wengi wamekuwa hawako tayari kutulia na kufanyia kazi ndoto zile wanazokuwa nazo, kwa kuzipa nafasi ndogo katika utekelezaji wake.
Kuna mamilioni ya watu ambao wanaamini wanaangamia kwa umaskini na kushindwa kwa sababu baadhi ya malengo waliyonayo wamekuwa hawawezi kuyafanyia kazi. Bila kujua watu wengi hujitengenezea mazingira mabaya kutokana na mawazo hasi ambayo yanachukuliwa na mawazo na kutafsiriwa kwenda katika vitendo.
Kama mwanamume au mwanamke ambaye amejenga katika mawazo yake utajiri na mafanikio na akafikia mafanikio hayo, ni hivyo pia kwa Wamarekani weusi ambao waliikabili meza ya kushindwa kwa maisha kwa sababu mawazo yao yalikuwa yamejenga picha ya umaskini, bahati mbaya na kushindwa. Lakini kwa sasa Wamarekani weusi hao wamepata mafanikio.
Kwa sasa hivi utaweza kutambua kwamba mawazo ni vitu ambavyo vikifanyiwa kazi vizuri na kutekelezwa vinaweza kuwekwa katika mfumo wa uhalisia. Kama utakuwa na njozi za kupata zaidi na ukazijengea picha hiyo bila kujali utakumbana na vikwazo gain, hiyo itakuwa ni vipaumbele katika maisha yako.
Kama utaruhusu picha ya namna hii kuwa ya kudumu katika ulimwengu wako wa mawazo; utafikiri mawazo ya mafanikio na kuzungukwa na watu wenye mafanikio watakaotia moyo njozi zako.
Utatenga sehemu ya kipato chako kwa ajili ya kujilipa wewe mwenyewe, moja ya hatua muhimu katika kupata utajiri. Utajihusisha katika mpango ambao unaleta mafanikio binafsi na kukufanya uchague lengo la maisha yako.
Pia utatafuta ujuzi na utaalamu kwa wale wote ambao wamefanikiwa. Mwishoni utafanikiwa licha ya kukumbana na vikwazo katika kutekeleza njozi zako.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 03

ASILI humpatia mtu kazi za kufanya pamoja na changamoto za maendeleo. Kwani sote tunajua kuwa maendeleo yoyote hutokana na juhudi. Na juhudi hiyo ndiyo inayomuimarisha mtu.
Maisha huwapendelea wale ambao wanaweza kuwa na msimamo juu ya kitu fulani, hata pale wanapokumbana na matatizo kwa sababu wakati mwingine ni lazima kupitia ugumu fulani. Hiyo ni sehemu ya changamoto za maisha.
Maisha siku zote ni changamoto. Elewa kuwa wewe si mtu pekee unayekabiliana na vikwazo hivyo katika maisha ya kila siku. Kumbuka unaishi katika dunia yenye changamoto.
Tuangalie mifano michache ya maisha ya watu wengi mashuhuri waliofanikiwa. Kwa mfano, Beethoven alipoteza uwezo wa kusikia kabla ya kutunga nyimbo nyingi ambazo kwazo anakumbukwa hata leo.
John Militon aliandika juu ya mbingu iliyopotea wakati akiwa kipofu.
Abraham Lincoln ambaye alikuwa mmoja wa marais wa Marekani, alilalazimika wakati fulani kukopa pesa kwa ajili ya nauli ya gari moshi kwa ajili ya kwenda kujitambulisha yeye mwenyewe.
Na baada ya kutafuta kazi yenye malipo mazuri kwa miaka mingi, Albert Einstein aligundua nadharia ya ‘relativity’ wakati akifanya kazi kama karani katika ofisi moja. Nadharia hiyo inasema kuwa vipimo vya mwendo nafasi na wakati vinawiana au kukadiriana. Nadharia hii imekuwa mashuhuri sana hata leo.
Marian Anderson ambaye hadi leo amebakia katika historia kuwa mwanamke aliyekuwa na sauti nzuri na nyororo, alipata mafanikio baada ya baba yake kufanya kazi ya kutembeza makaa ya mawe katika mitaa ya Phildephia ili aweze kupata ada ya kumsomesha muziki.
Hakujawahi kuwa na mtu mwenye mafanikio au kipaji ambaye hakuwahi kufahamu juu ya kushindwa hapo kabla, kuchanganyikiwa au kukabiliana na kipindi kigumu.
Wakati ambapo hakukuwa na pesa au ilikuwa adimu, wakati ambapo anakosa mguso wa ubinadamu, wakati mawazo mapya yanapokoma, au wakati mwili wako au hisia zinapokuwa zimefikia ukomo. Ishara ya mafanikio ni uwezo wa kukabiliana na hayo yote na kuyashinda huku yakikuacha wewe ukiendelea kuwepo.
Kuchanganyikiwa, kukata tamaa na wakati mwingine majonzi vinaweza kukuongoza katika furaha na mafanikio. Mara nyingi wale wote ambao hushinda wakati mgumu ni wanaume na wanawake ambao mwishoni hupata mafanikio makubwa na hawa ndiyo ambao wanatuhamasisha.
Katika mada hii, ningependa tujadiliane kanuni ambayo ukiifuata hutashindwa katika maisha yako. Kwa kuifuata kanuni hiyo unaweza kuongeza ubora na utajiri katika maisha yako, hatimaye kukufikisha katika malengo unayoyatarajia.
Pasipo tabia hiyo, huwezi kufurahia utajiri kwa jinsi yoyote ile. Kwa kanuni hii, matarajio mengine yataimarika na kufikia bidii zako na kufanikisha malengo yako yote. Tabia hii itakupa amani katika moyo wako, ambayo kamwe haitapeperusha mawazo yako. Kanuni hiyo ninayoiongelea ni ya msimamo.
Kuwa na msimamo maana yake ni kusadiki, shauku, uvumilivu na ujasiri katika kipindi unachokumbana na vikwazo mbalimbali. Zaidi ya yote inamaanisha kuwa usikate tamaa, usijiondoe na kamwe usikubali kushindwa.
Nguvu ya kuwa mtu wa msimamo ni tabia iliyoko kwa wanaume na wanawake wengi, ambao wamefanikiwa kwa kiwango kikubwa. Hahihitaji kuwa na akili sana ya mtu msomi, mwenye kipaji au rasilimali ni vile kuwa na malengo, bidii na uimara ambao utakupeleka kwenye mafanikio makubwa yako binafsi.
Wote waliofanikiwa katika maisha ni wale ambao wamekuwa wakifanya jitihada mbalimbali za kutaka kuwa na mafanikio, ambao hawakupenda kuamini kuwa wana vipaji, lakini ambao wameamua kuwa wanaweza kufanikisha jambo lolote lenye thamani, hiyo ni kutokana na kuwa na msimamo pamoja na jitihada.
Mwanafalsafa Epictetus alichunguza kuwa, “si vitu peke yake vinavyowasumbua wanaume, lakini ni uamuzi kuhusu vitu hivyo.” Maisha ni mwendelezo wa kukua na usafi, yenye changamoto na vikwazo.
Ni njia ya kuchuja udhaifu, uvivu na mambo yote yasiyovutia – yeyote yule asiye imara au anayekataa kujisimamia kwa nia ya kufanikiwa mara zote kanuni hiyo inakuwa mbaya kwake muda wote.
Mtu anayejituma binafsi anapaswa kuelewa kuwa kuna vikwazo mbalimbali mara zote katika maisha ambavyo anastahili kuvishinda. Waliofanikiwa wamekabiliana na changamoto hizo kwa haki na wana nguvu za kutosha, malighafi ya kutosha, na uthabiti unaotosha kuwazuia kuingia kwenye hatari hiyo ya kushindwa.
Uzoefu unaonyesha kuwa, mwanadamu huwa hatulii anapokaribia kuwa na mafanikio na wakati anapojiona anashindwa, hujitahidi kuondokana na hali hiyo ya kushindwa. Hivyo hutulia na kuanza kufikiri malengo yake ya mafanikio.
Anapofikiri kwa utulivu anagundua kuwa kushindwa si kitu, kinachotakiwa ni kuongeza jitihada katika kufikia malengo yake aliyoyapanga kwa kuweka mipango mipya ya kuweza kufanikiwa.
Mara nyingi hali ya kushindwa inatokana na mipaka ambayo watu wamejiwekea katika akili zao, kama watakuwa wajasiri na kupiga hatua moja mbele zaidi, watafanikiwa.
Kwa kawaida, hali ya kushindwa inawaathiri watu wengi katika njia mbili. Kwanza inawasaidia kama changamoto kubwa ya kupata mafanikio au inapunguza nguvu na kuwavunja watu moyo kwa nia ya kujaribu tena.
Walio wengi wamekuwa na matumaini ya mafanikio, wengine kuachilia na kupata dhiki katika nafsi zao kabla ya kujaribu. Pia inasemekana kuwa hali ya kushindwa inamfanya mtu kuwa na mipango mipya katika maisha ya mafanikio.
Somo kubwa katika maisha ni kujifunza ni jinsi gani ya kutumia fursa uliyonayo ya kupata ushindi kutoka katika hali ya kushindwa. Hiki ni kipimo cha kutofautisha wote waliofanikiwa na wote wasiofanikiwa.
Kiongozi hatakiwi kukata tamaa kutokana na kushindwa, lakini wakati wote anatakiwa kuwa na msukumo wa mafanikio. Kwa kuangalia kushindwa kwako, itajulikana kama kiongozi huyo anafaa kuongoza.
Wakati mwingine utakapokabiliana na kushindwa, kumbuka kuwa kila changamoto unayoipata na taabu inachukuliwa kama mbegu yenye faida. Anza kuitambua hiyo mbegu na kuipanda kupitia vitendo. Utagundua kuwa hakuna hali ya kushindwa katika maisha mpaka pale utakapoikubali hali hiyo.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 04

MTU mmoja aliyejulikana kwa jina la Frederick Douglas, alisema kuwa bahati yako ipo mkononi mwako. Na endapo utaitafuta, ni lazima utaiona.
Douglass anamaanisha kuwa mtu yeyote anayependa mafanikio na kuamua kupambana ili kufikia malengo yake, anafanikiwa. Hiyo ni kutokana na jitihada pamoja na bidii anayoionyesha mtu huyo.
Mtu yeyote ambaye hatataka kujikwamua kutoka katika hali ya dhiki aliyonayo, atabakia kuwa maskini na tegemezi. Utajiri wa watu wale wanaofanya jitihada na hata kufanikiwa hautamsaidia mtu ambaye hapendi kujishughulisha.
Kama hautajikwamua katika hali ya dhiki uliyonayo, kuendelea na ujinga wa kutotaka kujifunza ili kuondoka katika tabu yako, wenye akili watatumia juhudi na maarifa yao na kukuzidi katika hali ya kuwa na mafanikio. Kama utakuwa mwenye upumbavu, busara za wengine hazitakuongoza. Kama utapoteza muda na pesa zako, uchumi wa wengine utafikia kikomo na kukufedhehesha.
Unapokuwa na mafanikio yako binafsi unakuwa na nguvu katika kufanikisha mambo yako mbalimbali unayoyatarajia, na ndiyo maana kila mtu peke yake anafanya jitihada za kutaka kujikwamua kutoka kwenye umaskini.
Katika jamii tunayoishi, kila mmoja wetu ni mjasiriamali. Kila mmoja ni rais katika shirika lake. Hivyo atawajibika katika mafanikio na kushindwa kwa ofisi hiyo.
Wewe na familia yako ni wadau katika shirika lako, na ni jukumu lako kuhakikisha kuwa thamani ya mahitaji ya biashara zako yanakuwepo kwa miaka yote.
Wakati unaendelea kuendesha kampuni yako inayoendelea kukua, inawezekana kupunguza mahitaji makubwa kwa kusimamia vizuri pesa ulizonazo, kusimamia vizuri suala la uzalishaji, mauzo na kufanya utafiti.
Pasipokuwa na mtaji wa kutosha, hakuna uzalishaji. Bila uzalishaji, kampuni yako itakuwa haina kitu cha kuuza. Bila bidhaa, shirika lako litasimamisha uzalishaji. Na bila utafiti, washirika wako hawatakuwa na imani ya kuendelea kuwepo katika kampuni hiyo kwa siku zijazo.
Suala la kutumia akili yako ya kuzaliwa ni la muhimu sana. Utafiti unaonyesha kuwa mara nyingi mtu anayefanikiwa ni yule ambaye anatumia akili yake katika kumpatia faida.
Mfano, mtu mmoja alikopa pesa benki na kuweka dhamana kwa kutumia samani zake za nyumbani. Na alitumia akili yake kuwaza biashara atakayoifanya kutokana na mkopo ule. Alianzisha biashara ya kuuza nafaka kwa jumla na sasa hivi mtu huyo ana malori ambayo yanapeleka mizigo nje ya nchi.
Kufanikiwa kwa mtu huyo kusikufanye na wewe ukaanzisha biashara kama yake, kwani unaweza kukwama. Kinachotakiwa ni kuchekecha akili yako na kuamua kufanya biashara ambayo utaimudu.
Mafanikio katika biashara yako na kifedha yanakuja kutokana na uongozi mzuri katika kampuni yako unayoisimamia. Hakuna milango iliyo wazi katika suala la mafanikio, ni lazima ufanye utafiti, uweke malengo na kutimiza ndoto yako uliyoipanga. Japo kuna misuko suko mbalimbali katika kufikia mafanikio hayo.
Ukosefu wa nafasi isiwe sababu ya kutoa udhuru katika mipango yako inayoshindikana kutokana na kuwepo kwa vikwazo mbalimbali unavyoviruhusu wewe mwenyewe.
Kila maisha unayoyaishi yana nafasi nzuri ya mafanikio. George anasema tunaishi katika dunia ambayo wakati wote ina uwezekano wa kuwa na utajiri mwingi.
Maisha ni somo, na kila somo, linapokujia ni nafasi kwako ya kujifunza. Kila biashara unayoipitia ni nafasi kwako ya kujifunza. Unapowaza juu ya watu unaowafahamu waliofanikiwa, hiyo ni nafasi nzuri kwako ya kujifunza kutoka kwao.
Uwepo wako ni upendeleo wa pekee wa kukufanya uongeze bidii katika mipango yako, na pale unapopata bahati hiyo, nafasi yako ya mafanikio inakuja kwa haraka.
Mtu mwenye mafanikio, mvumbuzi na muasisi ni wale wenye ujasiri na wanaweza kusema, ndiyo, ninaweza! Njia ipo pale na nitaitafuta. Wote hao ambao binafsi wameyakubali maisha na changamoto zake na kuzifanyia kazi changamoto hizo katika mafanikio.
Acha kulalamika kutokana na bahati mbaya uliyokumbana nayo au jambo baya lililokupata, amua kuwa na nafasi ya kubadilika.
Kuna kitu kimoja ambacho unaweza kukifanya vyema zaidi ya mtu mwingine. Ni nini hicho? Tafuta mpaka pale utakapopata eneo lako ambalo utafanya vizuri na kuzidi wengine. Halafu upange mipango yako ukinuia kuwa utafanikiwa.
Kamwe usipende kuwa mtu wa kushindwa ila wewe ndiye unayeweza kupata mafanikio. Inawezekana kabisa mtu aliyezaliwa katika familia maskini, akakua katika hali ya umaskini, akasoma kwa shida na matatizo mengi, hatimaye mtu huyo akaja kuwa tajiri mkubwa.
Mifano mingi tunayokutana nayo ni ya watu walioishi katika hali duni, kutokana na hali ile wakaamua kubadilika na kuwa watu tofauti katika dunia tunayoiishi na wengi wao wamefanikiwa, ni matajiri wanaishi maisha ya raha.
Watu hao mara zote wamekuwa wakiwausia watoto wao kuishi maisha ya kujituma na kufanya bidii ili watakapokua waweze kuwa na mafanikio, pia wasitegemee utajiri wa wazazi wao.
Kamwe usikate tamaa, wala kuvunjika moyo. Utavuna kesho kile ulichokipanda leo.
Kila siku unatakiwa kujiuliza: “Siku hii ya leo kwangu ina maana gani?” utakapofanya maamuzi juu ya siku hiyo, utakuwa tayari kwa kutumia uzoefu ulionao wa kufanya jambo lile ambalo umelipanga.
Umepewa saa 24 kwa siku, siku saba kwa wiki, unatakiwa kuwajibika katika siku hizo. Uko huru kufanya kazi katika muda uliojipangia kutokana na uchaguzi wako.
Uamuzi wa mafanikio upo kwako, hivyo usivunjike moyo katika hatua unayoichukua ya kufanikisha malengo yako.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 05

MWANAFUNZI mmoja alimuuliza mwalimu wake ni ‘nini kinachompata mtu anayeamua kukaidi utendaji kazi wa kanuni ya dhahabu ‘Golden Rule”, mwalimu alikuwa na jibu rahisi tu kwa mwanafunzi huo.
Kama unataka kufahamu kile kinachotokea kwa mtu ambaye huamua kukaidi msingi ambao kanuni ya dhahabu inafanya kazi, chagua mtu mmoja katika jamii unayoishi anayeishi kwa lengo moja tu la kujikusanyia mali lakini akiwa hana ufahamu wowote wa jinsi mali hiyo inavyokusanywa.
Mchunguze mtu huyo na utagundua kuwa hakuna uchangamfu, hakuna ukarimu hakuna neno karibu katika mazungumzo yake. Kwa hakika amekuwa mtumwa kwa hitaji lake la fedha; amekuwa mbinafsi mkubwa pale linapokuja suala la kuwashirikisha wenzake ili nao wafurahie utajiri wake.
Itakuwa ni upumbavu wa hali ya juu kulinganisha mafanikio na mtu wa jinsi hiyo. Kwa hakika hakuwezi kuwa na mafanikio bila ya kuwapo furaha na hakuna mtu anayeweza kuwa na furaha bila ya kuwafanya watu wengine kuwa na furaha.
Ingawa utumiaji wa nguvu unaweza kuleta mafanikio katika maeneo mengi bado haiwezi kusababisha kuwapo uhusiano wa kudumu. Wakati mtu mwingine anapokupenda, anapocheka nawe, anapokubaliana nawe, hapo ndipo unapoweza kuwa na hakika kuwa mtu huyo atafikiri nawe atakusaidia na atashirikiana nawe. Haiba yenye mvuto ni moja ya kati ya nyenzo muhimu za kijamii.
Lakini ni nini siri ya kuwa na haiba yenye mvuto. Naamini tunawafahamu watu ambao huonekana kuwavutia wengine, marafiki, wateja au watu ambao wanakutana nao katika shughuli za kimaisha.
Mara nyingi huwa tunaishia kusema kuwa watu hawa wana mvuto au bahati na watu hao wanaowavutia kiasi cha kufikiri kuwa huenda kuna nguvu ya asili inayosababisha hali hiyo. Dhana ya jinsi hii si sahihi kabisa kwani huwezi kumlazimisha mtu fulani anapenda au kuvutiwa na mtu mwingine.
Lakini kinyume cha dhana hiyo unaweza kuwavuta watu kwa kukidhi njaa katika mahitaji ya msingi yaliyo katika maisha ya mwanadamu. Kisa hiki kinafunua siri ya dhana hii.
Mfanyabiashara mmoja nchini Marekani amabaye alikuwa wa asili ya Afrika aliwasili ofisini kwake mapema ikiwa ni saa kadhaa kuliko ilivyokuwa kawaida yake. Siku hiyo alikuwa na shughuli ambazo alihitaji kuzikamilisha kabla ya wafanyakazi wake hawajawasili kazini.
Kwa muda huo aliowasili hakukuwa na mtu mwingine isipokuwa kijana mmoja aliyejulikana kwa jina la George aliyekuwa ni mwangalizi wa ofisi. George alikuwa mfanyakazi mwaminifu aliyekuwa akitoa huduma kwa kampuni ile. Wakati ule bosi wake alipokuwa akiingia ofisni , george alikuwa katika shughuli ya kuzoa taka na kufuta vumbi katika samani za ofisi.
Bosi alipogundua hilo alimwambia maneneo haya: “George, unajua ninapoangalia jengo hili nashindwa hata kufikiri na kueleza jinsi ambavyo umekuwa rasilimali muhimu katika kampuni kwa miaka yote hii ambayo umekuwa mtumishi hapa. Umefanya eneo hili kuwa safi na la kuvutia kwa wafanyakazi pamoja na wateja wetu jambo ambalo limewafanya wafurahie.
“George,” bosi aliendelea “Wewe ni sehemu muhimu katika kampuni hii na ningependa utambue kuwa ninathamini yote ambayo umekuwa ukifanya.”
George alisita kidogo na kisha akajibu kwa kusema: “Asante bosi” kisha akatoka nje huku akiwa ameshikilia kitambaa ambacho alikuwa anakitumia kufuta vumbi.
Dakika chache baadae mlango wa ofisi ulifunguliwa na alikuwa ni George tena. Macho yake yalionekana kulengwalengwa na machozi, jambo ambalo lilimshangaza bosi wake kiasi cha kuuliza “Je kuna tatizo gani George, je nimesema neno lolote ambalo limekuudhi?”
George alijaribu tabasamu kisha akasema “Hapana bosi, hujaniudhi kwa lolote. Lakini nina jambo ambalo ningependa kushirikiana na wewe.”
Ukimya ulitawala chumba kwa muda mfupi baadae George akasema maneno yafuatayo. “Unajua bosi nimefanya kazi na kampuni hii kwa miaka 17 kati ya hiyo 12 ikiwa ni chini yako na asubuhi hii ya leo ndiyo mara ya kwanza mtu kuniambia kuwa anathamini kile ambacho nimekuwa nikifanya.”
Baadaye George aliendelea kusema hivi. “Ninapenda bosi utambue kuwa ninathamini kile ambacho umekisema kwangu asubuhi hii ya leo kuliko vile ambavyo nimekuwa nikithamini hundi ya mshahara wangu! Nilipenda ujue hilo.” Baada ya kusema maneno hayo George aligeuka na kutoka ndani ya chumba cha bosi wake.
Jambo muhimu katika asili ya mwanadamu ni hitaji la kuthaminiwa. Mtu hawezi kutoa kilicho bora kwa kubadilishana na fedha tu, lakini anaweza kutoa kila kinachowezekana kwa ajili ya kuthaminiwa tu hata kama ni kwa kiasi kidogo kiasi gani.
Pale unapoamua kutokosoa, kulaumu na badala yake ukaamua kuangalia kila uwezekanao wa kutamka kwa dhati japo neno moja tu la kusifia au kuthamini, utagundua kuwa watu wengine watatamani kuandamana na wewe.
Kwa dhati kabisa watataka kuwa jirani na wewe. Kwa kufanya iwe tabia yako kusifia kwa dhati na uaminifu utakuwa umepiga hatua muhimu katika kujenga na kupalilia mafanikio na furaha yako mwenyewe.
Hebu jaribu kujiuliza maswali haya. Je, unapata kusifiwa na watu wengine, je, watu wanakubaliana na kile unachokifanya au kukisema, je, wanathamini mchango wako nyumbani au kazini? Je, ni lini ulimsifia kwa dhati mtu mwingine au kutoa maneno ya dhati katika kuthamini kazi au manen yake? Mambo haya mawili huenda kwa pamoja na ni vigumu kuyatenganisha. Watu wengi hivi leo wanaonekana kuchanganyikiwa.
Huku wakiwa waliozidiwa na shughuli nyingi katika miji na majiji makubwa, wamejikuta wakitawaliwa na hisia na mihemko. Wakati hisia zetu ana mihemko vinaposhindwa kudhibitiwa, tutajikuta tukiwatendea wengine kwa haraka, tukionyesha ishara na kufanya maamuzi ya haraka huku tukitumia maneno ambayo hayakuchaguliwa kwa uangalifu unaostahili.
Jaribu kuweka kando hisia zako za ndani. Na kanuni muhimu ni hii simama, sikiliza, fikiri na utafakari wewe mwenyewe. Kwa namna nyingine ni sawa tungesema kuwa jaribu kuhisi kwa jinsi ambayo watu wengine wanajihisi, na si vile ambavyo wewe unajihisi.
Ni wazi kuwa unapojiangalia katika kioo unachotarajia kukiona ni taswira yako. Vivyo hivyo mtu mwingine angependa kuona taswira yake kutoka katika kioo chako, hisia zake na mtazamo wake.
Jaribu kufikiri juu ya ufahari, hisia na mihemko ya wengine na si kwako tu. Hapo utashangaa kuona jinsi watu wengi watakavyovutiwa nawe na kutaka kuwa jirani nawe wakati wote. Na hapo ndipo utakapogundua thamani na umuhimu wa kuwatendea watu wengine kwa jinsi wanavyojihisi na kujisikia badala ya vile wewe unavyofikiri na kujisikia.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 06

ILI kufikia malengo halisi ni lazima uwe na haiba ambayo inalingana na viwango fulani. Wachache miongoni mwetu tumezaliwa na haiba inayong’aa na yenye mvuto, lakini inawezekana tukawa tumeruhusu mitazamo hasi na tabia zisizo na mvuto kuweza kuchafua mwonekano ambao haiba yetu inaweza kuwa imeujenga hapo awali.
Hata hivyo bado tunaweza kung’arisha mwonekano wetu wa nje ambao umefifia na kuweza kukuza hisia za wale wote ambao tulikutana nao kama tutapenda kufanya hivyo kwa nia ya dhati.
Nini hasa kujenga haiba yenye mvuto? Kitabu kitakatifu cha Biblia hutoa mwongozo mzuri. "Watendee wengine vile ambavyo nawe ungependa kutendewa,” tamko hilo linaonekana mara kadhaa kwa njia tofauti katika imani mbalimbali za dini pamoja na falsafa mbalimbali.
Kwa usahihi zaidi, msemo huo hujulikana kama kanuni ya dhahabu 'Golden Rule'. Mimi na wewe tunalazimika kuwapo katika dunia inayokaliwa na wengine pia na hivyo ni lazima tutambue namna ya kuishi nao.
Vile tunavyowakabili na kuwatendea watu wote wa jamii na vile ambavyo jamii hiyo inaitikia dhidi yetu kwa kiasi fulani hutegemeana na vile tunavyojisalimisha katika mamlaka ya kanuni hii.
Maisha ni kioo. Vitu vyema huvutia watu wema. Vile ambavyo tunatarajia wengine watuitikie ndivyo ambavyo ni lazima tujieleze.Bila shaka umewahi kusikia ikisemwa kuwa tabia ya mtoto hufunua au kuelezea vile anavyotendewa.
Kama anatendewa kwa upendo atakuwa mwenye kupenda, iwapo anatendewa kwa ukatili na kwa njia ya matusi, basi na yeye atakuwa mkatili na mwenye tabia ya kutukana. Kwa kiasi fulani kuna ukweli ndani yake kuwa tunapa kutoka kwa wengine kile tunachotoa. Na huu ndio msingi wa haiba yetu.
Maisha ni kioo ambacho huakisi mwonekana wako. Kama unatabasamu, basi maisha yataakisi furaha na uchangamfu. Iwapo ni mtu mwenye kisirani na hasira, basi maisha yataakisi hali na picha halisi ya jinsi ulivyo. Kwa asili, kile unachokisema juu ya wengine pia husemwa juu yako.
Huwezi kupata kitu katika dunia hii ambacho hujakipata kutoka kwako kwanza. Asili hujielezea kutokana na mihemuko yako. Kama unafurahi, dunia itafurahi. Kama una uaminifu, basi utaaminiwa. Kama unapenda, basi jua unapendwa. Kama unachukia, jua pia kuwa unachukiwa. Hivyo kimsingi tambua kuwa unachovuna ni kile ulichopanda.
Wanaume na wanawake wengi duniani hutumia kanuni hiyo ya dhahabu ili kujumuisha yale yote waliyoyahitaji kwa kadiri wanavyotembea katika barabara kuyaelekea mafanikio. Mwanamuziki mmoja aliyejulikana kama Leontyne Price alisimulia kisa cha ajabu juu ya namna kanuni hii ilivyobadilisha maisha yake.
Anasema kuwa katika miaka ya 1960 alikuwa ni mwalimu mara baada ya kuhitimu masomo ya chuo kikuu cha Ohio. Anasema ingawa alikuwa amefaulu kwa kiwango cha juu, bado alikuwa hajafikia malengo yake. Huku akiwa mwenye huzuni, kufundisha kulionekana kumpatia changamoto kidogo. Aliwapenda wanafunzi wake, japo wakati mwingine alionekana kama mwenye kuchoka. Lakini akafikiri, kwanini iwe hivyo? Wakati akiwa mtoto aliweza kujifunza kusoma maandishi ya muziki kabla hata ya kujua kusoma vitabu. Kuimba ndiko kulikuwa mapenzi yake na sauti ya ndani ikamuita, jambo ambalo lilimfanya anyong’onyee na kukata tamaa kwa kudhani kuwa haliwezekani.
Japo kwa siri aliazimia kuanza kutazama uwezekano wa kuingia katika uimbaji, na mara akaanza kuzuru kumbi za maonyesho. Siku moja wakati akitoka shuleni aliwakuta watoto wakicheza na alijikuta akiwaangalia kwa muda mrefu. Alipenda watoto lakini pia alipenda kuimba. Hapo alijikuta akiwa njia panda, akiwaza juu ya tamu na chungu na iwapo aendelee kufundisha au aache na kwenda kuimba.
Licha ya walimu wenzake kumsihi sana asiache kazi ya kufundisha, aliamua kutii mapigo na matakwa ya moyo wake na siku iliyofuata aliamua kuwasilisha barua ya kuacha kazi ya ualimu.
Wakati wote alipotafakari juu ya njozi zake Leontyne alijiona kuwa na sifa zinazostahili kuwa mwanamziki nyota lakini alibaki kuwa na swali moja kuwa ataweza kutimiza ndoto hizo?
Baadaye aligundua kuwa ili aweze kutimiza lengo lake anahitaji kuongeza ujuzi na hilo lilihitaji pesa au ikiwezekana mfadhili. Huku akitawaliwa na nia mpya iliyokuwa ndani yake, wazazi wake waliamua kuunga mkono uamuzi wake wa kuimba. Hata hivyo kulingana na kikwazo cha kiuchumi, baba akiwa fundi muashi na mama mkunga, waliweza kutoa msaada wa hali tu na si mali. Ilikuwa ni wazi kuwa bila ya kuhudhuria madarasa ya muziki, kusafiri maeneo mbalimbali, na gharama nyingine, kazi yake ingekuwa ni ngumu. Hata hivyo utashi wa kanuni ya dhahabu hautambui mipaka au vikwazo.
Kipindi cha nyuma hata kabla ya kujiunga na masomo ya Chuo Kikuu Leontyne alikuwa na wakati wa furaha wakati akiwa nyumbani kwao mjini Mississipi pamoja na marafiki zake wa karibu wawili ambao waliishi jirani na nyumba yao. Ingawa wakati na hali ya maisha ilikuwa imewatenganisha, marafiki hawa kwa kipindi kirefu hisia zao na kukumbukana vilikuwa ni vitu vilivyodumu.
Alipofanikiwa kumtembelea rafiki yake huyo huku akitarajia kukutana na ukalimu na furaha zile walizokuwa nazo wakati wakiwa wadogo na karibu alijikuta akilakiwa na mama wa rafiki yake ambaye alikuwa mkarimu na aliyekumbuka urafiki wa mabinti hawa wawili.
Leontyne hakusita kumwelezea mama wa rafiki yake juu ya ndoto na malengo yake, hakusita kuonyesha huzuni iliyokuwa ndani yake kutokana na kung’amua kuwa alilazimika kuanza kufundisha tena baada ya kuona kuwa ndoto yake ya kutumbuiza mamilioni ya watu iko mbioni kuyeyuka.
Kabla Leontyne hajainua mkono wake ili kufuta machozi yaliyokuwa yakitiririka katika macho yake, mama huyo mkarimu aliahidi kumfadhili binti huyo ili kumsaidia kuendelea na masomo yake ya muziki na hatimaye aweze kutimiza ndoto yake ya kuwa muimbaji mahiri.
Hata hivyo msaada wa mama huyo uliambatana na masharti. Alimuambia Leontyne kuwa angemsaidia tu iwapo atakubaliana na wazo kuwa atakapofikia malengo yake na yeye ahakikishe kuwa anakuwa mkono wa msaada kwa yeyote atakayehitaji na angefanya hivyo kwa kumpasia kanuni ya dhahabu, jambo ambalo Leontyne alikubaliana nalo kwa moyo mweupe.
Leontyne ameishi kwa uaminifu na kutimiza makubaliano ambayo alifanya na mama wa rafiki yake na kwa hakika amekuwa msaada mkubwa kwani ameweza kuwasaidia wasanii wengi ambao walihitaji msaada ili waweze kufikia malengo katika maisha yao na kukamilisha njozi ambazo walikuwa nazo.
Na hapo kanuni ya dhahabu ikawa na maana kwake kuwa alipenda kutendewa vyema na wengine kama alivyofanya mama wa rafiki yake na yeye amepaswa kuwatendea wengine hivyo, na hapo ndipo ule msemo wa unachokitoa kwa wengine ni kile ambacho umekipokea kutoka kwa wengine unapotimia.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 07

ILI haiba iweze kuwa na mafaniko ni lazima idumu huku ikifanya kazi ya kutambulika ya Daniel James inataja ukweli kuwa haiba yenye mvuto si tu inaweza kufungua milango mingi bali inaweza pia kukusaidia ili uweze kuwa na kiwango cha juu cha ufanisi.
James alikulia katika nyakati za giza za huko Frorida nchini Marekani ambapo kulikuwa na ubaguzi wa rangi katika mji huo.
Miaka michache baadaye aliweza kushinda ubaguzi wakati akiwa katika jeshi baada ya kuwa Mmarekani mweusi wa pili kupandishwa cheo na kuwa Jenerali katika Jeshi la Anga la Marekani na kuwa mtu wa nne katika historia ya utumishi wa jeshi.
Utajiri na mafanikio ya James vilitokana na uwezo wa kuweza kutumia kikamilifu ushauri ambao mama yake alishirikiana naye wakati alipokuwa mtoto.
“Mama yangu alinifundisha misingi,” alikumbuka. “Upendo wa Mungu, upendo wa nchi na upendo wa mwanadamu. Na si kujaribu kuwa makini katika kukosoa kwamba umesahau kuangalia katika mazuri ambayo yako kwetu sisi wote.
“Kwa baadhi ya watu utahitajika kuchimba sana ili kuweza kupata sifa nzuri, lakini kila mtu anastahili pongezi na kuthaminiwa”.
Licha ya kukosekana haki ambako nimekumbana nako nilifahamau thamani ya kuthamini. Kama ningejazilizia sifa na kuthamini wafanyakazi wenzangu, nilijikuta kuwa nilikuwa na furaha ya kufanya hivyo.
James aliambatana na hekima hii maisha yake yote alikuwa na uwezo wa kuwafanya wale wote waliokuwa kando yake wajihisi kuwa ni maalumu kwa kuwatambua mmoja baada ya mwingine kwa kile kizuri walichofanya.
Alipuuzia ile dhana ya kwamba watu wengi unaokutana nao hujihisi kuwa ni bora zaidi yako kwa namna fulani. Aliamua kuugawa moyo wake kwa ajili ya wale waliokuwa wadogo kwake kwa kutambua umuhimu wao na mchango wao.
Aliwapa kile walichohitaji na mara nyingi ilikuwa ni kusifu kwa uwazi na uaminfu pamoja na kuthamini.
Ninaamini kuwa hutadharau mifano hii rahisi, lakini pengine zawadi yenye maana sana ambayo unaweza kuitoa kwa mtu mwingine nayo si nyingine isipokuwa kuthamini.
Kama bado unafikiri kuwa una mashaka juu ya dhana ya kwamba kusifu na kuthamini vina nguvu ya kimiujiza basi hebu jifunze katika mfano huu.
Kisa hiki kinaweza kuwa sawa na kilichopitwa na wakati lakini ujumbe wake unaonekana kuwa mbele ya wakati. Ilikuwa ni kawaida ya mtu mmoja mzee kukaa nje ya ukuta wa mji wa kale wa hapo alipokuwa akiishi akifanya kazi ya kuangalia wapita njia ambao walikuwa wakija kutoka upande mmoja na kuishia katika upande mwingine.
Kwa kawaida alipendelea kukaa katika kivuli akiwa amezungukwa na watoto akiwasimulia hadithi walizozipenda. Katika muda mwingi wa mchana wapita njia wengi wangependa kusimama hapo na kuzungumza naye.
Siku moja wakati wa majira ya joto mgeni moja alifika hapa na kuamua kusimama kwa muda ili aweze kuzungumzia na yule mzee ambaye kwa wakati wote huo alikuwa makini akiwasimulia hadithi marafiki zake watoto.
Mgeni yule alimsogelea mzee yule na kumuuliza: “Ninafikiria kuhamia katika mji wako huu je, unaweza kuniambia ni watu wa aina gani ambao wanaishi katika mji huu?”
Haraka mzee yule alisema, “Ni aina gani ya watu huishi katika mji ambao wewe unatoka?” yule mgeni alijibu kwa kusema: “Watu katika mji wangu si wakarimu, wanadanganya na kuiba na kusema uongo. Wanazungumza vibaya kila mmoja juu ya mwingine. Ninaondoka katika mji huo kwa sababu ya watu wasiofaa ambao wanaishi huko.”
Yule mzee alimwangalia mgeni yule kisha akasema: “Ninasikitika kukufahamisha kuwa utakutana na watu wa aina hiyo hiyo katika mji huu.” Na bila ya kusema neno lolote mgeni yule aligeuka nyuma na kuondoka zake na kumuacha yule mzee akiendelea na kuwasimulia watoto hadithi.
Muda mfupi baadaye mgeni mwingine akaja hadi katika lango la kuingilia katika mji huo, naye pia akasimama na kuanza kuongea. Akasema: “Mtu wangu mwema, ninahitaji kuingia mjini huu wa kwako je, unaweza kuniambia ni aina gani ya watu ambao wanaishi humo ndani?”
Yule mzee akauliza swali kama lile la mwanzo alilomuuliza yule mgeni wa mwanzo. “Ni aina gani ya watu ambao wanaishi katika mji ambao wewe unatoka?” Mgeni yule akajibu kwa kusema kuwa “Watu katika mji wangu ni wema sana. Wana urafiki na kila mtu wana upendo na wakati wote huwa wanaangalia uwezekano wa kutenda mambo mema kwa ajili ya watu wengine. Nilisikitika sana kuondoka katika mji ule kutokana na ukarimu na utu wema wa watu wake lakini hata hivyo kazi ninayoifanya inanilazimu kuondoka katika mji ule.”
Mzee yule alimshika mkono mgeni yule na kumwambia: “Utapata watu wa jinsi hiyo hapa. Karibu katika mji wetu.” Mgeni yule akatembea na kuingia kupitia katika lango la mji.
Watoto walikaa kimya. Baadaye mmoja wao alimsogelea mzee yule na kumuuliza “kwa nini babu hukuwaambia watu wale ukweli? Ulimwambia mmoja kuwa watu wetu walikuwa ni wabaya na mwingine kuwa watu wetu ni wazuri.” Mzee aliwaomba waketi ili aweze kuwaeleza.
“Nimewaambia ukweli,” alisema. “Mnaona, bila kujali kuwa mnakwenda wapi au mnafanya nini mtakuta aina ya watu mnaowataka katika jamii nyingine. Kama unataka watu wazuri mtawapata, lakini pia kama mnatafuta watu wabaya mtawapata pia bila shaka ndio mtakaopata. Kila mmoja wetu hapa ana sifa nzuri zaidi ya mbaya alizonazo. Siku zote jaribu kutafuta kilicho chema kutoka kwa watu wengine”.
Wakati fulani mtu mmoja alisema: “Ninajua furaha ni nini kwa sababu nimeshafanya kazi njema.” Mtu huyo alisema hivyo kwa sababu alifanya kazi nzuri na akapata kuthaminiwa na kusifiwa na wenzake kutokana na kile alichofanya.
Kutambua, kusifu na kupenda ni vitu vyenye kutia hamasa sana katika maisha. Tunapokumbana na vitu hivyo huwa tunaondoka katika eneo hilo ambalo tumekutana navyo tukiwa na furaha na kujihisi wenye thamani.
Kinyume chake ni kwamba tunapokosolewa huwa tunajihisi kuwa hatujitoshelezi na tusio na mwelekeo. Kwanini tunajisikia furaha pale tunaposifiwa? Ni kwa sababu kusifiwa maana yake ni utambulisho na uthibitisho wa thamani yetu.
Sifa huonyesha hutuambia kuwa tunaheshimika, tunahitajika na kuthaminiwa na hivyo kuonyesha kuwapo kwetu. Mara kadhaa huwa tunazuia sifa.
Wakati mwingine ni kwa sababu tunataka kuonekana kama wazalendo zaidi au wabinafsi zaidi. Lakini katika wakati mwingine hata hatuahangaiki kufanya juhudi.
Tunasahau kuwa kila mmoja hufurahia kutambauliwa, neno la kumsifia. Kusifia ni uthibitisho wa thamani yetu. Kusifu ni kukaririsha ushuhuda kuwa hisia zetu za ndani zimehalalishwa. Hutuambia kuwa tunahitajika.
Hivyo basi sifia wengine lakini pia usisahau kujisifia wewe mwenyewe pale unapostahili. Sifia maisha. Ni rahisi sana na jambo lenye kufurahisha kushiriki katika maisha ya mtu mwingine kwa kusema maneno machache lakini yenye kujenga.
Kusifu kwa dhati huhitaji nguvu kidogo sana na hufanyika kwa muda mfupi. Lakini matokeo yake huonekana baada ya muda mfupi lakini yakadumu kwa muda mrefu.

FIKIRIA UTAJIRI SEHEMU YA 08

“HAKUNA mtu anayependa kuwa masikini,”
maneno hayo yalisemwa na George Shaw. Naye Sophie Tucker anasema: “Nimeshakuwa tajiri, nimeshakuwa maskini, katika hali zote hizo maisha ya utajiri ni mazuri.
Kuna aina ya mafanikio mtu anayoyapata bila kutumia fedha. Pia kuna mafanikio mengine ili yapatikane inabidi uwe na fedha, inategemeana ni wapi unapoanzia ili kufikia malengo yako unayokusudia.
Fedha au utajiri ni jambo ambalo tunalipata kutokana na juhudi mbalimbali ambazo zinatufikisha kufikia malengo tuliyokusudia katika fikra zetu.Kwanza inapasa kujipanga na kujua jinsi gani utafanyia kazi fedha hizo ili kufikia malengo na matarajio yako.
Watu wengi wanasema kuwa pesa inaleta afya. Pia ukumbuke kuwa furaha ya kweli haipatikani kutokana na vitu ulivyonavyo, bali inapatikana kutokana na jinsi ulivyo, pamoja na uwezo wa kuweza kutumia malighafi uliyo nayo. Unaweza kuwa na fedha ili mradi kufurahia uhuru wa mwili na akili.
Mtu hawezi kuwa huru kama atakuwa anafanya kazi ya mfululizo kila siku na kupata kipato kidogo, endapo mtu huyo itamlazimu kulipa zaidi ya kile anachopata, mfano analipa gharama kubwa.
Katika mfululizo huu utaelewa njia ya kukufanya uwe huru kutoka kwenye vikwazo unavyokabiliana navyo na kufurahia maisha ya utajiri.
Njia ya kwanza ni muhimu kama unazika, mara moja , ile hali ya kuona kuwa pesa ni mbaya au haina umuhimu. Pesa siyo mbaya. Kama Biblia inavyosema, “kupenda pesa ni kubaya.” Ni kweli kuwa, pesa ni muhimu. Ni muhimu kama chakula na nguo kinavyohitajiwa kununuliwa, malazi, elimu na ankara unazotakiwa kulipia.
Pesa ni muhimu kwa yeyote anayeishi katika jamii ya waliostaarabika, na kufikiri kuwa si muhimu ni kujidanganya.
Kumbuka kuwa ni haki yako kuwa tajiri. Pesa ndiye dereva wetu mkubwa, inaongeza mtandao wako wa kuwa tajiri, inakuwezesha kupata utajiri ili uweze kuwasaidia wengine, na kumiliki fedha kwa faida itakusaidia wewe na familia yako kuwa na malengo ya mafanikio. Uwezekano wa kuwa na pesa unachangamsha akili yako kufikiria kufikia malengo uliyojiwekea.
Pia ni kawaida kuwa huwezi ukawa na furaha kama wewe ni maskini, na unahitaji kutokuwa maskini. Umaskini au kutokuwa tajiri ni aina ya maumivu yanayosababishwa na upumbavu wa mtu wa kuzijua kanuni katika akili yake ambazo zitamwongoza katika mafanikio.
Umaskini ni uchafu, unakufanya kutokuwa huru, pia unadhoofisha ujuzi ulio nao. Uko katika aina ya ugonjwa. Mtu maskini anajiona kama mfungwa, umaskini unawafanya wanaume na wanawake kupenda kunywa pombe, kula madawa ya kulevya na mara nyingine kujinyonga.
Umaskini unafanya kitu chenye thamani, kipaji, watoto wenye akili kugeuka na kufanya uhalifu. Unawafanya watu kufanya mambo ambayo hawajawahi kufikiria kama wangeyafanya.
Utajiri si pesa tu, bali hata amani uliyonayo ni utajiri. Amani katika akili yako ni jambo la thamani lenye mafanikio. Katika hali yoyote ile unapokuwa na amani, unakaribisha utajiri katika maisha yako. Pia inakusaidia kuishi maisha yako katika maeneo yako mwenyewe unayoyapenda. inakupatia amani katika kile unachochagua, ndiyo maana maisha yako kila siku yanakuwa ya kitajiri na yenye mafanikio.
Mtu mmoja alisema kuwa utajiri unakuja kwa mtu ambaye anaona umuhimu wa utajiri. Kama maelezo yaliyotangulia yalivyosema, huwezi kuwabeba wengine kuelekea mafanikio, lakini unaweza ukawaonyesha njia ya kila mmoja kujisaidia mwenyewe.
Je, ni kiasi gani cha pesa ambacho unataka kukimiliki? Chukua dakika chache na ujibu maswali yafuatayo.
Umepata nini kwa ajili ya kufanya biashara? Dunia imekufanyia nini kwa kile unachokifanya? Watu wangapi wanafanya kile unachokifanya? Utakapojibu maswali hayo, utajua ni kwanini baadhi ya watu wanakuwa na pesa nyingi zaidi ya wengine?
Kwa hiyo unatakiwa kuondoa mawazo yote uliyonayo juu ya umaskini, yanayokuzuia usisonge mbele kimaendeleo.
Umaskini si adui. Adui ni mtu ambaye wakati wote anaangalia si tu udhaifu alionao bali anauabudu pia.
Amekuwa akitumia nguvu zake kuwashawishi wenzake kuwa hakuna chochote wanachoweza kukifanya wakafanikiwa.
Ondoa kabisa mawazo yako potofu kuwa ni lazima uwe maskini. Kumbuka umaskini na mafanikio unatokana na akili yako. Kama utaamua kufuta mawazo ya umaskini, ni lazima uielekeze akili yako kwenye bahati njema, mafanikio na kufaulu. Kumbuka kuwa siri uliyoigundua ni sawa na shamba la almasi. Hii habari inaelezea siri kubwa ya maisha kwamba una shamba kubwa la almasi. Hizi almasi zilizopo zinajulikana kama jambo lenye kuwezekana na uwezo. Kuna uzuri mwingi wa vito vya thamani ndani yake, inatakiwa subira ili uweze kuchimba.
Ujuzi katika maisha yetu ya kila siku juu ya suala la kufikia malengo yenye mafanikio, unafundisha kuwa thamani ya sheria nyingi zinazosisitizwa katika kufikia malengo yako na kuwa tajri ni elimu.
Kwa kuwa elimu itakufanya kuwa mwelewa. Pili, kuwa mdadisi. Unapokuwa mdadisi uwapo shuleni, kazini au katika jumuiya. Jifunze kutoka kwa wengine, walimu wako, familia yako na rafiki zako. Kila mmoja ana kitu tofauti kwa ajili ya mwingine.
Tatu, amua ni nini unachohitaji nje ya maisha unayoyaishi. Kabiliana na changamoto mpya zinazokutatiza. Nne, kuwa tayari kupata faida katika nafasi zote zinazotokea kwako. Si tu kwa zile nafasi zinazogonga katika mlango wako. Kuwa wa tofauti.
Tano, usichukie. Chuki haizalishi. Wala haitakujengea chochote katika maisha yako. Na katika yote hayo, kuwa mkweli wa nafsi yako.
Kuwa mtu wa thamani na uligundue hilo. Jiamini. Kila siku uwe na maono mapya ambayo ni imara.
Fikiri uwe tajiri imefikia tamati.
Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine mpya.

About the Author

Hello,I am Web Designer and Expert facebooktwitteryoutubeinstagramexternal-link

Chapisha Maoni

Cookie Consent
We serve cookies on this site to analyze traffic, remember your preferences, and optimize your experience.
Oops!
It seems there is something wrong with your internet connection. Please connect to the internet and start browsing again.
AdBlock Detected!
We have detected that you are using adblocking plugin in your browser.
The revenue we earn by the advertisements is used to manage this website, we request you to whitelist our website in your adblocking plugin.
Site is Blocked
Sorry! This site is not available in your country.