MOYO ULIOJAA MAUMIVU
SEHEMU YA 44
Theo hakuwa na habari, alifika mahali hapo kwa kazi moja tu. Aliwaona wanawake wote kuwa sawa, kichwa chake kilikuwa na mawazo juu ya familia yake na yale mambo yote ambayo walikuwa wakipitia.
Kushuti video hiyo ilichukua saa nne ndipo wakapumzika kwa ajili ya kupata chakula. Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi ya Iyanya kumfuata mwanaume huyo na kutaka kuongea naye. Haraka sana akasimama alipokuwa na kuanza kumsogelea.
Wapambe wake walipomuona, wakamzuia lakini Theo akawaambia wamuache kwani kusingekuwa na tatizo lolote lile kama angekaa na msichana huyo na kuzungumza naye.
Kwa Iyanya hiyo ikaonekana kuwa kama bahati, alikuwa na nafasi moja maishani mwake, nafasi ambayo ingempa hatma ya maisha yake kwa mwanaume huyo, hiyo nafasi alitakiwa kuitumia kwa umakini sana, yaani kama angeshindwa hiyo, basi asingeweza kupata tena.
Alimwangalia Theo, akamsogelea na kukaa karibu naye huku wakila. Moyo wake ulikuwa na furaha mno, alimpenda mwanaume huyo kupita kawaida, alitamani kumwambia kile kilichoujaza moyo wake muda huo lakini akaamua kutulia kwanza.
“Hii ni nafasi ya bahati sana kuwa katika video yako,” alisema Iyanya huku akimwangalia mwanaume huyo ambaye kwa mbali alionekana kutokuwa sawa.
“Kwa nini?”
“Wewe ni maarufu sana. Nadhani kupitia video yako nitakwenda kupata jina,” alisema Iyanya huku akiachia tabasamu pana, kwa jinsi alivyokuwa mzuri, uzuri wake ukaongezeka maradufu.
Theo hakujibu kitu zaidi ya kuachia tabasamu tu.
Alimwangalia msichana huyo, ni kweli alikuwa mrembo lakini hiyo haikuwa sababu ya kutaka kulala naye kwa sababu alijiheshimu sana, kubwa zaidi alimuheshimu mno mke wake.
“Theo! Ninahitaji msaada wako!” alisema Iyanya huku akimwangalia Theo.
“Msaada gani?”