MOYO ULIOJAA MAUMIVU
SEHEMU YA 39
Aliumia moyoni mwake, kile alichoambiwa hakutakiwa kukisikia kabisa, alikumbuka jinsi alivyoishi na mume wake, walivyokuwa na mipango mingi kuhusu watoto wao, walipanga mambo mengi, waliwafanyia shopping, waliwanunulia kila kitu mpaka kuwaandalia majina lakini mwisho wa siku, kila kitu kilionekana kwenda hovyo.
Theo ndiye alikuwa mfariji wake pekee, alilia sana lakini mwanaume huyo alikuwa pembeni yake na kuanza kumbembeleza kwa maneno mengi ya kutia moyo, maneno ambayo aliamini yangeweza kumsahaulisha mke wake juu ya watoto wake hao.
“Violeth! Usilie, hutakiwi kumkufuru Mungu. Kumbuka kila kitu kinachotokea ni mipango ya Mungu, kulia sana inamaanisha kwamba unakosoa kazi zake alizozifanya. Nyamaza, kama amemchukua mtoto wetu mmoja, ametuachia mmoja kwa sababu zake, naomba umshukuru Mungu kwa kila jambo,” alisema Theo kwa sauti ya chini, karibu kabisa na sikio la mke wake.
“Ninaumia sana...moyo wangu unaumaaaa....” alisema Violeth.
“Najua! Nimeumia pia kama wewe unavyoumia ila kuumia kwangu, machozi yangu hayawezi kumrudisha Harry! Naomba unyamaze mpenzi....” alisema Theo huku akimbembeleza mke wake huyo.
Mwisho wa siku Violeth alitakiwa kukubaliana na ukweli wa kile kilichotokea, kwamba mtoto wake mmoja alifariki dunia na kubaki mmoja.
Waliendelea kufarijiana mpaka pale walipokabidhiwa mwili wa mtoto wao na kwenda kuuzika katika makaburi yaliyokuwa nyuma ya hospitali hiyo.
Stori kuhusu kile kilichotokea zikaanza kusambaa kila kona, watu waliwaonea huruma, kila mmoja alisikitika mno kwani walikumbuka namna mwanamke huyo na mume wake walivyokuwa wakiwaambia kuhusu mapacha hao, jinsi watakavyotokea kuwapenda na kuwalea katika malezi mazuri lakini mwisho wa siku hawakufanikiwa kuwa na watoto wote wawili.
Watu wakawatumia salamu za pole, waliguswa na wengine kwenda kuwatembelea nyumbani kwao. Kwenye mitandao ya kijamii, ni stori kuhusu familia hiyo tu, ndiyo walikuwa watu maarufu kuliko mastaa wote nchini Tanzania hivyo hata viongozi wa serikalini na watu wengine wote waliwapa pole kwa kile kilichokuwa kimetokea.